Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Hamis Mohamed Mwinjuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muheza

Primary Question

MHE. HAMIS M. MWINJUMA aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha upatikanaji wa soko la machungwa?

Supplementary Question 1

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pia nashukuru kwa majibu ya Serikali kupitia kwa Naibu Waziri ambayo yananipeleka kwenye maswali mawili madogo ya nyongeza. La kwanza, wakati huu ambao taratibu mbalimbali zinaendelea za kutafuta masoko kwa ajili ya machungwa, lakini pia kutafuta uwekezaji kwa ajili ya kutengeneza viwanda cha kuchakata matunda: Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kutengeneza vituo vya ukusanyaji, uhifadhi na uuzaji wa machungwa ili kuwapa uhakika wa sehemu ya kuuzia machungwa yao wananchi wa Wilaya ya Muheza na pia kuepusha idadi kubwa ya machungwa yanayoharibika kila mwaka kwa kukosa uhifadhi mzuri?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hamis Mohamed Mwinjuma, Mbunge wa Muheza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia sana kuhusiana na soko la machungwa katika Mkoa wa Tanga Wilayani Muheza. Niseme kweli, machungwa ya Muheza ni ya aina yake kwa maana ya ladha; ni matamu kuliko; kwa hiyo, unaweza ukayatenganisha kuliko ya maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imeanza mpango wa kujenga maghala ambayo yatakuwa kama vituo vya kukusanyia matunda ili kuhakikisha matunda hayapotei. Siyo maghala tu, yatakuwa ni maghala ambayo yatakuwa na vyumba vya ubaridi (cold rooms) ambavyo vitawasaidia wakulima kutunza mazao yao, yakae kwa muda mrefu wakati wanatafuta masoko.

Mheshimiwa Spika, moja ya jitihada kama nilivyosema ni kujenga viwanda vya kuchakata matunda ya machungwa, lakini tunavutia viwanda vidogo na vikubwa. Tumeshaanza kujenga viwanda vidogo kupitia vikundi vidogo vidogo ambavyo vitaongeza thamani. Pia tumeshaanza kuongea na wawekezaji wakubwa ambao wataenda kuwekeza kwenye eneo la Muheza kwa kuwapa vivutio maalum maana wengi wanataka kuwekeza mjini badala ya mashambani ambako ndiko kwenye machungwa. Kwa hiyo, tutaweka mkakati maalum wa kuwavutia ili wapate vivutio vya kuwekeza katika Mkoa wa Tanga hususan Muheza. Nakushukuru.