Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Primary Question

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha matokeo ya tafiti za kilimo yanawafikia wakulima?

Supplementary Question 1

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ninaipongeza Serikali kwa hatua hizi zinazofanya za kuwafikia wakulima, lakini hatua hizi ambazo wamezichukuwa zinalenga hasa wakulima wakubwa. Kama mnavyojua, wakulima wa Tanzania wengi wao wana uchumi mdogo, ni wakulima wadogowadogo ambao wanalima heka moja, nusu heka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni mkakati gani hasa Serikali inao wa kuwafikia wakulima wadogo ambao hawana uwezo wa kununua simu, hawana uwezo wa kununua TV au kuweza kufika kwenye warsha na maonesho ya Nanenane. Je, Serikali ina mkakati gani hasa wa kuwafikia? (Makofi)

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu niliyoyatoa kwenye swali la msingi, Serikali inachukuwa hatua mbalimbali: Moja, sasa hivi tumeanza kusajili wakulima, kwa muda mrefu tumekuwa tukihudumia watu tusiowatambua. Kwa hiyo, sasa hivi tumeanza process ya kuwasajili wakulima kuwatambua walipo, kuchukua hadi fingerprints, vilevile tunaenda kuchukua GPS coordinate za mashamba yao, zoezi hili linaendelea.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tunalolifanya ni kumwezesha Afisa Ugani ili awe na uwezo wa kuwafika wakulima. Tunao upungufu wa Maafisa Ugani katika nchi yetu wasiozidi Elfu Saba, kwa hiyo ili kuhudumia kaya Milioni Saba inakuwa tatizo. Kwa hiyo, Serikali imewekeza kuwapatia pikipiki na sasa tunawapatia nyezo na hivi karibuni tutawapatia vishikwambi ambavyo vitakuwa vinachukua taarifa za kila mkulima aliyemtembelea katika eneo lake. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge hii extension program itatuchukua kwa kipindi cha miaka mitatu ili kuweza kufika kule ambapo tunapotaka na kutambua mkulima ni nani na kila Afisa Kilimo kukabidhiwa idadi ya wakulima atakaokuwa anawahudumia kwa siku. (Makofi)