Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Bahati Keneth Ndingo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Primary Question

MHE. BAHATI K. NDINGO aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaweka mfumo utakaoruhusu wafungwa kupata haki ya faragha na wenza wao?

Supplementary Question 1

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza; swali la kwanza; ni mifumo ipi ya kisheria ambayo mpaka sasa haijatengenezwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, mchakato huo utachukua muda gani ili wafungwa wetu waweze kupata haki ya msingi na tumpunguzie haki balozi wa afya ya akili?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali yote ya nyongeza ya Mheshimiwa Bahati Ndigo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba ieleweke kwamba suala la tendo la ndoa si haki ya msingi, ni haki lakini si haki ya msingi. Haki ya msingi ambayo tunatoa kwa wafungwa, chakula malazi, mavazi kwa hiyo, kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi kwamba kuna mambo ya kuzingatia ambayo yanapaswa kuzingia kwanza kabla ya kuruhusu haki hiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge anapigania.

Mheshimiwa Spika, hata ukiangalia katika nchi zilizoendelea basi utaratibu huo haupo kama hivyo, kuna utaratibu ambao wale wafungwa wanapelekwa kwenda kutembelea familia, siyo inafanyika katika magereza, lakini ukitaka ifanyike magereza unahitaji kwanza uangalie miundombinu, mila zetu na desturi. Kwa sababu wakati mwingine inakuwa siyo jambo jema kwa mila zetu na desturi, kwamba kila mtu anajua sasa hawa wanakwenda kufanya tendo la ndoa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa maelezo hayo naomba Mheshimiwa Bahati aridhikena majibu yangu ya msingi.

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. BAHATI K. NDINGO aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaweka mfumo utakaoruhusu wafungwa kupata haki ya faragha na wenza wao?

Supplementary Question 2

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ni kwa nini Serikali isiweke utaratibu wa kuwawezesha mahabusu au wafungwa kupata fursa ya kuzungumza na familia zao angalau mara moja kila baada ya miezi mitatu, kuliko hivi sasa unaongelea kwenye nondo, unakuta hakuna usikivu wowote ule?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la namna ya kuboresha utaratibu wa kuzungumza aidha wenza wao na familia zao ni jambo ambalo linazungumzika. Kimsingi tukubaliane kwamba sasa hivi utaratibu huo upo, labda Mheshimiwa Esther yeye haridhiki na ile frequency ama muda. Sasa hilo linategemea na mambo mengi, mazingira, kwa sababu masuala ya magereza yanazingatia usalama, kwamba watu walioko ndani na watu wanaokuja, ni lazima mazingira ya magereza iendelee kulindwa kiusalama ili wanaokuja wasihatarishe usalama wa magereza na wafungwa walioko ndani. Ndiyo maana utaratibu huo umewekwa kwa sasa hivi, lakini pale ambapo miundombinu itaruhusu na pengine utaratibu wa kuweza kuwaona mara kwa mara si jambo baya, lakini nadhani ni jambo linalotakiwa kuangaliwa na kutafakariwa kulingana na usalama wa magereza yetu.

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. BAHATI K. NDINGO aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaweka mfumo utakaoruhusu wafungwa kupata haki ya faragha na wenza wao?

Supplementary Question 3

MHE. EMMANUEL MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Magereza zetu zimekuwa na tatizo ambalo linatokana na hili swali la msingi kwamba kwa kuwa hawa watu wanakosa faragha, wengine wanafanya vitendo wenyewe kwa wenyewe mle magerezani. Je, Serikali ili kupunguza hivyo vitendo vya watu kugeuzana wenyewe kwa wenyewe magerezani, inachukua hatua gani kupunguza vitendo hivyo ambavyo vinasababisha kuwa kinyume hata na mila na desturi zetu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuna njia nyingi ambazo Serikali inachukua, la kwanza ni kuhakikisha tunaimarisha ulinzi katika magereza na kuimarisha ulinzi kuna njia nyingi vilevile, tuna mifumo ya ki-intelligence kupata taarifa kabla matukio hayajajitokeza. Pia kuna utaratibu ambao kuna askari waliopo katika magereza kuangalia mienendo na mazingira ya wafungwa katika magereza na tabia zao vilevile.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi ni kwamba kupitia Serikali ya Awamu ya Sita, kuna mikakati kabambe ya kufanya maboresho makubwa katika vyombo vyetu vya usalama. Moja ni kuhakikisha tunaimarisha na kuboresha miundombinu ya magereza ili kutenganisha kati ya wafungwa kwa mfano, kutenganisha wafungwa wenye umri fulani mpaka umri fulani, wenye historia ama rekodi ya uharifu zaidi kuliko wengine na mambo mengine, ili kutoa nafasi kwa kuweza kupeleka nguvu zaidi ya uangalizi katika maeneo ambayo yanastahili kulingana na uzito na changamoto ya mfungwa husika.