Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA aliuliza: - Je, Serikali haioni umuhimu wa kurudisha masomo ya ziada ya kazi za mikono kama vile useremala, upishi, ushonaji, kilimo na ujenzi katika shule za msingi na sekondari ili kupunguza changamoto ya ajira?

Supplementary Question 1

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Namshukuru Mheshimiwa Waziri na naipongeza sana Serikali kwa kupokea mashauri mengi ya Waheshimiwa na kuyafanyia kazi. Hata hivyo, nina maswali mafupi mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, ni lini Serikali sasa itaweza kukamilisha mapitio hayo na kazi hii kuwa nzuri zaidi kwa manufaa ya vijana wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa vile Baraza la Mitihani la Taifa (NECTA) pamoja na Elimu ya Juu ni masuala ya Muungano: Je, Serikali haioni umuhimu wa kushirikiana na Wizara ya Elimu Zanzibar ili manufaa ambayo watayapata vijana wetu wa Tanzania Bara na Zanzibar waweze kupata? (Makofi)

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba sasa kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Giga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la uratibu au upitiaji upya wa mitaala yetu ni agizo la Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati akihutubia Bunge tarehe 22 Aprili, 2021. Nasi kama Wizara, baada ya maagizo yale, tulianza kuyafanyia kazi kwa haraka. Nimhakikishie Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba kazi ile inaendelea vizuri na tumeanza kukusanya hayo maoni; tulianzia pale Dar es Salaam, baadaye tukaenda Zanzibar na baadaye tulifanyia hapa Dodoma na kazi hiyo bado inaendelea. Kazi hii inatarajiwa kukamilika baada ya miaka mitatu na miezi tisa. Tunatarajia mtaala huu mpya utaanza kutumika ifikapo Januari, 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo la pili ambalo amezungumzia namna gani Wizara hizi mbili katika maeneo haya, namna gani yanaweza kufaidika? Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, eneo ambalo tupo tofauti na wenzetu wa Tanzania Visiwani ni katika eneo la elimu ya msingi; lakini upande wa sekondari tunatumia mtaala wa aina moja na upande wa Vyuo Vikuu tunatumia mtaala wa aina moja.

Mheshimiwa Spika, nimwondoe wasiwasi, wakati tunafanya mapitio ya mitaala yetu hii, tunashirikiana kwa karibu sana na Taasisi ya Elimu ya Zanzibar, nayo vilevile inafanya mapitio ya mitaala hiyo ili basi ile Tanzania tunayoihitaji iweze kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushuruku sana.