Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Neema Gerald Mwandabila

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga Vyuo Vikuu katika Mkoa wa Songwe?

Supplementary Question 1

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Nitakuwa na maswali mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoelekea, elimu ya Vyuo na Vyuo Vikuu inakuwa ni hitaji la msingi kwa wananchi na tunafahamu kabisa Mikoa ya pembezoni imekuwa inapata changamoto hiyo ya kupata huduma ya Vyuo na Vyuo Vikuu. Tunachofahamu Watanzania wengi ni masikini, hawawezi kwenda maeneo hayo wote na kupata hiyo, lakini tuna watumishi wetu wengi ambao wanahitaji kuendeleza ujuzi wao:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni kwamba, ni kwa namna gani Serikali isione umuhimu wa kuwa na mgawanyo sawa (equal distribution) wa vyuo kwa maeneo yote? Kwa Mikoa yetu kumekuwa na changamoto ya kwanza vyuo vyote vinaenda katika Makao Makuu ya Kanda, lakini kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi, Serikali inao uwezo wa kugawanya kwamba chuo hiki kijengwe sehemu fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ambacho nakiona, ni lini Serikali itaweza kuendeleza Chuo cha Miyunga (DIT) kiweze kutoa Shahada katika eneo lile? Ahsante.

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Mwandabila kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika jibu la msingi ni kwamba Vyuo vyetu Vikuu vinaanzishwa au kupelekwa kwenye maeneo kulingana na uhitaji. Nimkahikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba ipo miongozo ambayo imewekwa na Serikali na inatekelezwa na wenzetu wa TCU kwa niaba ya Wizara ya Elimu pindi wahitaji au taasisi zinapohitaji kufungua vyuo kwenye maeneo mbalimbali kuonesha maeneo yapi yenye uhitaji wa namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, kabla ya maeneo haya havijafunguliwa vyuo hivi, mara nyingi sana tunafanya assessment ambayo inaitwa need assessment ya kuhakikisha kwamba kweli tukipeleka chuo kwenye maeneo hayo, uhitaji huo utapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la pili, amezungumzia tawi letu la Miyunga kutoa Shahada. Chuo hiki cha Miyunga au Campus hii ya Miyunga ya DIT ilianzishwa mwaka 2017 ikiwa na malengo mahsusi. Malengo yake makuu ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunapata mafundi stadi na mafundi sanifu katika eneo la Uhandisi pamoja na eneo la uchimbaji wa madini. Masomo yanayotolewa hapa ni yale ya ufundi pamoja na ufundi stadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anazungumzia kutoa Shahada, lakini tunafahamu kwamba Taifa letu bado lina uhitaji mkubwa sana wa kada hizi za kati za ufundi pamoja ufundi sanifu. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya Serikali ni kuondoa changamoto ya mafundi sanifu pamoja na mafundi stadi wa kawaida. Kwa hiyo, kwa sasa kwa mwelekeo wetu na dhamira yetu ya Chuo kile ni kuhakikisha kwamba inakwenda kutoa kada hizo na kada ya Shahada bado tutategemea vyuo vingine vilivyopo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Name

Dr. Charles Stephen Kimei

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga Vyuo Vikuu katika Mkoa wa Songwe?

Supplementary Question 2

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ubarikiwe sana kwa kuniona. Swali langu linahusu Vyuo vya ufundi stadi vilivyopo kwenye Kata zetu kwenye Jimbo la Vunjo Kata ya Mwika, Kata ya Marangu, Kata ya Mamba na Kata ya Makuyuni Pamoja na Kiruavunjo ambavyo vimekufa. Naomba niulize, Serikali ina mpango gani wa kufufua vyuo hivi na kuvipa stadi mpya ambazo zitawawezesha wananchi wa Jimbo lile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mkakati gani kutuonesha kanzidata ya Vyuo vya Ufundi Stadi ambavyo vipo nchini ili tuweze kuwahamasisha wananchi wetu wakasome huko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Serikali ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na vyuo vya ufundi stadi katika kila Wilaya nchini. Vile vile Serikali inajikita kuhakikisha kwamba tunakuwa na vyuo vya ufundi stadi vya Mikoa na Kanda mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu, sasa hivi tumeanzisha vituo, zile center of excellence. Kwa mfano, kwa pale DIT Dar es Salaam tutakuwa na center of excellence katika masuala ya TEHAMA, Arusha eneo la Arusha Technical tuna center of excellence katika masuala ya nishati jadidifu, Mwanza tunaanza center of excellence katika masuala ya ngozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba Wilaya zote zitakwenda kupata vyuo hivi kwa sababu tumeona umuhimu na uhitaji wa vyuo hivi nchini. Vilevile tunajikita katika maeneo ya Mikoa sambamba na hivi vyuo ulivyovitaja, kwamba tayari sasa tupo katika tathmini ya kuhakikisha vyuo vyote vile ambavyo vilikuwa vimekufa zamani, tunaenda kuvifufua sambamba na kuanzisha vyuo vipya katika Wilaya zote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Pius Stephen Chaya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Primary Question

MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itajenga Vyuo Vikuu katika Mkoa wa Songwe?

Supplementary Question 3

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii. Kwa kuwa vijana wanaoenda chou kikuu ni wachache, hasa wale wanaomaliza kidato cha nne, ukilinganisha na wale wanaobaki. Je, ni nini mpango wa Serikali sasa wa kujenga chuo cha VETA cha ufundi katika Wilaya ya Manyoni? Ahsante sana.

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Chaya, Mbunge wa Manyoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyoeleza katika majibu ya swali la msingi na maswali mawili ya nyongeza, pamoja na yale maswali ya Dkt. Kimei; dhamira na nia ya Serikali na Sera yetu inazungumza kwamba, kila wilaya angalau tuwe na chuo kimoja. Tumeanza tayari mkakati huu na tumeanza kutekeleza katika wilaya 29 nchini. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Chaya awe na Subira katika kipindi hiki ambacho Serikali inaendelea kutafuta fedha, tutaifikia Manyoni, tumeanza na pale Ikungi na tukitoka Ikungi tutakwenda Manyoni kwa Mheshimiwa Dkt. Chaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chanya aondoe shaka, Serikali hii ya Awamu ya Sita iko hapa kwa ajili ya kutekeleza mahitaji yao. Tukitoka hapo tutaenda kwa Mheshimiwa Katambi kule Shinyanga kuhakikisha na Shinyanga nayo inapata chuo hiki. Ahsante. (Makofi)