Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Viwanda vya Kusindika Maziwa katika Mkoa wa Arusha?

Supplementary Question 1

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama Mheshimiwa Waziri alivyosema kwenye jibu lake la msingi Mkoa wa Arusha ni miongoni mwa mikoa, ambayo inaongoza kwa uzalishaji wa maziwa hapa nchini. Sio hayo tu maziwa yanayozalishwa katika Mkoa wa Arusha ni maziwa yenye viwango na ubora wa hali ya juu. Inasikitisha sana kuona bado Serikali hatujaweza kuwasaidia wafugaji na wazalishaji wa maziwa katika Mkoa wa Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika lita alizotaja Mheshimiwa Waziri hapa, lita milioni 30 ni lita milioni sita tu, ambazo zinakwenda kuchakatwa kwenye viwanda vyetu ni sawa na asilimia 20 tu. Asilimia 80 ya maziwa yanayozalishwa katika Mkoa wa Arusha yote yanapotea kwa sababu hayapiti kwenye viwanda kwa ajili ya kuchakatwa. Hii hapa inasababishwa na ukosefu wa maeneo ya ukusanyaji wa maziwa haya kwa ajili ya kupeleka katika viwanda vyetu. Swali langu kwa Serikali; je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka mipango madhubuti kwa ajili ya kuongeza hizi collection points hususani kwenye ngazi za chini ambazo uzalishaji ndio mkubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; katika Mkoa wa Arusha kuna Taasisi za Utafiti kama CAMARTEC na TEMDO. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongezea uwezo hizi taasisi kwa ajili ya kuendeleza sekta ya viwanda vidogo vidogo? Ahsante. (Makofi)

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango madhubuti na ndio maana kila mwaka tunahakikisha tunaongeza bajeti kupitia Wizara husika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, lakini pia na Wizara nyingine ili kuhakikisha tunaboresha sehemu za kukusanyia maziwa kwa maana ya collection centres.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kweli Taasisi za CAMARTEC na TEMDO ni Taasisi ambazo zinasaidia sana, teknolojia ambazo zinakwenda kuwasaidia vijijini kwa maana ya wafugaji na wakulima. Kila mwaka tunaendelea kuwaongezea bajeti ili waendelee, kuzalisha mashine au teknolojia rahisi na stahiki kwa ajili ya kusaidia wakulima wa vijijini ikiwemo wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.