Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Condester Michael Sichalwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Momba

Primary Question

MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Jimbo la Momba?

Supplementary Question 1

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini bado, changamoto ya maji kwenye Jimbo la Momba ni kubwa sana. Naomba kuiuliza Serikali niongeze maswali mawili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vijiji ambavyo umevieleza tunavyo vijiji 72 na vitongoji 302 inaonyesha kwamba hata nusu ya vijiji hivyo vitakuwa bado havijapata maji safi na salama. Ombi langu kwa Serikali, viko baadhi ya visima ambavyo vilishawahi kuchimbwa nyuma na wakoloni, vilishawahi kuchimbwa nyuma na wamishionari lakini pia na baadhi ya wakandarasi ambao walikuja kujenga barabara kwenye Jimbo la Momba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza, nini kauli ya Serikali kwenda kuvitembelea visima vile ambavyo vimeshawahi kufanya kazi vizuri huko nyuma kutokana bado kuna changamoto ya maji vinaweza vikatusaidia vikawa kama njia nyingine ya mbadala kutatua changamoto ya maji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kwa kuwa, baadhi ya vijiji ambavyo vimeonyesha vinao miradi hiyo ya maji lakini zipo Taasisi kama Vituo vya Afya, Zahanati pamoja na Sekondari havipati utoshelevu wa maji. Watoto wetu especially wa kike wameendelea kuteseka sana kufuata maji wakati mwingine zaidi ya kilomita 10. Mfano, Shule ya Sekondari Chikanamlilo, Shule ya Sekondari Momba, Shule ya Sekondari Uwanda, Shule ya Sekondari Ivuna, Shule ya Sekondari Nzoka na shule zingine 13 ambazo ziko ndani ya Jimbo la Momba pamoja na Zahanati na Vituo vya Afya kama Kamsamba na Kapele. Je, ni nini kauli ya Serikali kutuchimbia visima virefu ili Taasisi hizi ziweze kujipatia maji yake bila kutegemea kwenye vile vituo ambavyo tunang’ang’ania na wananchi na havitoshelezi? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Condester, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kutembelea visima ambavyo ni chakavu hii ni moja ya jukumu letu na tayari, Mheshimiwa Waziri amewaagiza watendaji wote kwenye mikoa yote, kwa maana ya Regional Managers (RMs) na Managing Directors (MDs) wasimamie visima vyote ambavyo ni chakavu. Vile ambavyo uwezekano wa kuvirejesha katika hali njema ya kutoa maji safi na salama vyote viweze kurejeshwa katika hali nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Jimbo la Momba sisi kama Wizara tumeshaleta Shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuchimba visima virefu. Hivyo, visima hivi ambavyo vya kukarabati lakini uchimbaji wa visima virefu kwenye swali lako la pili la nyongeza, navyo tayari vimeshaanza kufanyiwa kazi katika baadhi ya maeneo. Tayari visima vitano vimeshachimbwa kati ya visima 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, napenda tu kumtoa hofu Mheshimiwa Mbunge, kwamba sisi kama Wizara tutakwenda kuhakikisha katika sehemu zote ambako Taasisi za Serikali zipo kama zile Shule alizozitaja pamoja na Vituo vya Afya na Hospitali maji ni lazima yafike na huo ndio Motto wa Wizara. (Makofi)

Name

Cecil David Mwambe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ndanda

Primary Question

MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Jimbo la Momba?

Supplementary Question 2

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye Jimbo la Ndanda tuna mradi mkubwa wa maji uliogharimu zaidi ya shilingi bilioni tano uliokusudiwa kuhudumia Kata ya Mwena, Kata ya Chikundi pamoja na Kata ya Chikukwe. Hata hivyo mradi huu unafanya kazi kwa kiwango cha chini kabisa kwa sababu inaonekana ilikuwa ni poor designing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu kwa Mheshimiwa Waziri, je, haoni haja ya kuwaagiza wataalam wake wakakague mradi huu na kupeleka mapendekezo bora Serikalini, ili kuweza kuboresha ili wananchi wa Kata hizo wapate maji kwa kipindi chote cha mwaka?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi la kupeleka wataalam wakakague mradi huu na ni mradi ambao unakwenda kugharimu Serikali fedha nyingi zaidi ya Shilingi bilioni tano. Hii ni moja ya majukumu yetu Mheshimiwa Mbunge, tayari Mheshimiwa Waziri, amewasisitiza sana watendaji wanatakiwa kufuatilia hii miradi. Hivyo, nami napenda kusisitiza Managing Director na Regional Manager wa Mkoa wa Mtwara wahakikishe wanakwenda kusimamia huu mradi kuona unatekelezwa kadri ambavyo unapaswa kuwa. (Makofi)

Name

Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Jimbo la Momba?

Supplementary Question 3

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Changamoto ya maji iliyopo katika Jimbo la Momba haitofautiani na changamoto iliyopo katika Jiji la Dodoma, kwamba kuna baadhi ya maeneo yamekuwa yakikosa maji hata kwa wiki tatu kwa maelezo kwamba mitambo ya Mzakwe imezimwa kutokana na ukosefu wa umeme.

Napenda kufahamu, je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na kadhia hii ili kuwaondolea wananchi usumbufu wa kukosa maji mara kwa mara. Ahsante.(Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Naibu wangu kwa kazi nzuri na namna gani anavyojibu maswali hapa Bungeni. Hata hivyo, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge, lakini kwanza nimpongeze Mama yangu Toufiq, kwa kazi kubwa na nzuri anayofanya katika Mkoa huu wa Dodoma. Tukiri kabisa sisi kama Wizara ya Maji hapa Jiji la Dodoma kumekuwa na ongezeko kubwa la watu, uhitaji na uzalishaji wa maji katika Jiji la Dodoma uwezo wa mtambo wetu ni lita milioni 60 na mahitaji yake ni lita milioni 103 kutokana na ongezeko kubwa la watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa hiyo maelekezo mahususi ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa Wizara yetu ya Maji, kwa sababu lazima tumtue mwana mama ndoo kichwani. Tunakwenda kuyatoa maji ya Ziwa Victoria na kuja kuyaleta katika Jiji hili la Dodoma, ili kuhakikisha kwamba tunaondokana na changamoto hii. Kwa mkakati wa muda mfupi tunaendelea kuchimba visima virefu katika maeneo mbalimbali, ili kuongeza uzalishaji kwa muda mfupi na wananchi waendelee kupata huduma ya maji. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Jimbo la Momba?

Supplementary Question 4

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Jimbo la Tabora Mjini ni kati ya Majimbo ambayo yamenufaika na Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria, lakini mpaka sasa baadhi ya maeneo ya Jimbo hilo hayana maji kabisa. Je, Serikali imekwama wapi kusambaza maji kwa wananchi wa Tabora Mjini? (Makofi)

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa, kutoka Tabora kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi ule mkubwa kutoka Ziwa Victoria ni mradi ambao ni endelevu na ni mradi wenye manufaa makubwa sana. Maeneo mengi ambayo yamekuwa yanapaswa kupitiwa na mradi ule yataendelea kupata maji kwa wakati wote. Kwa maeneo machache ambayo kama bado hayajapata maji, wataalam wetu wanaendelea kufanya kazi kuhakikisha usambazaji wa maji ni zoezi endelevu. Hivyo waendelee kuvuta subira muda si mrefu na wao watapata maji. (Makofi)

Name

Neema Gerald Mwandabila

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika Jimbo la Momba?

Supplementary Question 5

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa swali la nyongeza. Ni wazi Wizara hii imekuwa ikifanya kazi kubwa kuhakikisha huduma ya maji inafika katika maeneo mengi. Katika maeneo ya Majiji, Manispaa na Miji kumekuwa na changamoto ya milipuko ya moto. Ambapo ukiuliza unaambiwa visima vya maji ambavyo vitajaza kwenye magari maji kwa wepesi havipo. Swali langu nilitamani kufahamu ni nini mkakati wa Wizara kuhakikisha katika project, kila mradi unaokuwa unaandaliwa kunakuwa na setting ya visima au matanki ambayo yatajaza maji kwa haraka katika magari ya zimamoto? Ahsante.

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mwandabila, kutoka Songwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili swali aliloliuliza ni utekelezaji wa Wizara ya Mambo ya Ndani na hawa wenzetu wa Zimamoto wanaufahamu wajibu wao. Taasisi zote za Serikali ambazo zinahitaji huduma ya maji wanafahamu wanapaswa kufika katika ofisi zetu kwenye mikoa yao. Ili waweze kuongea na wataalam wetu na kuona njia njema ya kutumia ili waweze kupata huduma ya maji katika ofisi zao. Taasisi zote za Umma zinapeleka maji kwa gharama zao na pale inapobidi kupata huduma ya kiupendeleo basi huwa wanafika na kuweza kueleza tatizo husika. Hivyo, wenzetu wa Zimamoto wanafahamu wapi wafike ili waweze kufanya vyema. (Makofi)