Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapa maeneo ya uchimbaji wachimbaji wadogo wa Kata za Nyarugusu, Nyaruyeye na Kaseme?

Supplementary Question 1

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Ni kweli kwamba Serikali imeweza kujibu kwamba itawapa maeneo wachimbaji wadogo katika maeneo hayo, lakini imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana hasa katika eneo la Nyarugusu maeneo ya STAMICO, kila wakati Serikali imekuwa ikiahidi kwamba itawapatia maeneo na wananchi wanahitaji kujua kwamba ni lini sasa Serikali itawapatia maeneo haya ya wachimbaji wadogo hasa maeneo ya Nyarugusu? (Makofi)
Swali la pili, mwaka 2015 Serikali ilizindua mradi mkubwa sana wa wachimbaji wadogo pale Rwamgasa na tuliuzindua mradi huu kwa vigelele na shangwe, lakini sasa hakuna kinachoendelea mpaka sasa. Ni mradi wa World Bank! Napenda kujua, ni lini sasa mradi huu utaanza rasmi ili wachimbaji wadogo waweze kunufaika?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa Serikali imekuwa ikikusudia kuwatengea maeneo wananchi, hasa wa eneo la Mheshimiwa Bukwimba. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Bukwimba, amekuwa akifuatilia sana maeneo ya wachimbaji wadogo katika eneo lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, mwaka 2015 kwa juhudi zake ambazo aliomba wananchi wachimbiwe maeneo, walitengewa maeneo 95, eneo la Rwanyamgaza. Kadhalika, maeneo ya Kaseme, walitengewa maeneo 43.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba tu Mheshimiwa Bukwimba awahamasishe wananchi, kwa sababu kati ya maeneo 95 aliyotengewa, ni maeneo 25 tu kule Rwanyamgaza yanafanya kazi; na kati ya maeneo 43 kule Kaseme ni maeneo 17. Hata hivyo Mheshimiwa Bukwimba kwa juhudi zako bado tunakutengea maeneo mengine ambayo yanaachiwa wazi na wananchi hasa eneo la Buziba. Buckreef itaachia hekta 200, lakini bado Kampuni ya ARL itaachia hekta 100; bado Kampuni ya Bismak itaachia hekta 120, lakini na Ernest Masawe ataachia hekta 90, hiyo ni kwa ajili ya wananchi wako Mheshimiwa Bukwimba. Kwa hiyo, bado tunakutengea maeneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini sasa? Mwezi wa Kumi tunaanza kutenga maeneo rasmi. Hii ni kwa nchi nzima ikiwemo eneo la Igunga kule Iborogero, maeneo ya Kibao kwa Mfipa, maeneo ya kule Mkuranga kwa ajili ya Waziwazi lakini na maeneo mengine ya Busiri, pamoja na Londani Sambalu kule Singida kwa Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, bado tunaendelea kutenga maeneo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala lake la pili ni kwamba Kituo cha Kuchenjua Madini kwa ajili ya wachimbaji wadogo, kimechukua muda mrefu. Mheshimiwa Bukwimba nakupongeza sana, tuna kituo kimoja tu cha mfano cha kuchenjua madini hapa nchini na ndiyo kituo cha Rwamgasa ambao Mheshimiwa Bukwimba, mwaka 2015 na mwaka 2014 ulihangaika sana. Mheshimiwa Bukwimba nakupongeza sana, utakuwa ni Mbunge wa mfano kwa sababu ndiyo eneo tunalofungua Kituo cha Kuchenjua cha Mfano hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini kinakamilika sasa? Leo tumefungua tenda kwa ajili ya kumpata mjenzi na kazi ya kujenga itaanza mwezi Septemba mwaka huu na mradi ule utakamilika mwezi Mei mwakani. Gharama yake ni hela nyingi kidogo, ni Dola 800,000, tutazitenga ili kituo hiki kianze kufanya kazi. Pia nawapongeze mgodi wa GGM nao wanachangia Dola 200,000. Kwa hiyo, kituo hiki kitaanza kufanya kazi lakini mantiki ya kituo hiki kitasaidia sana wachimbaji wadogo kujua thamani sasa ya dhahabu wanayochimba hapa nchini.
Mheshimiwa Naibu Spika, nawahamasisha wananchi wote ambako madini yanachimbwa sasa wote tupeleke kwenye eneo hili la Rwamgasa ambacho Mheshimiwa Bukwimba amekifungua ili wananchi wetu sasa wanufaike na rasilimali yetu ya dhahabu.

Name

Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapa maeneo ya uchimbaji wachimbaji wadogo wa Kata za Nyarugusu, Nyaruyeye na Kaseme?

Supplementary Question 2

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Naitwa Ikupa Alex, samahani. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, wachimbaji hawa wadogo nchini ni muda mrefu sasa wamekuwa wakikumbwa na migogoro ya mara kwa mara na wachimbaji wakubwa hasa kule Mererani. Je, Serikali ina mpango ama mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inatatua migogoro hii na kuhakikisha kwamba haijirudii tena?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa wachimbaji wadogo wadogo na siyo Mererani peke yake ni kote nchini, wamekuwa wakikumbwa na migogoro hasa kati yao na wawekezaji wakubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Mererani, kwanza kabisa kuna migogoro ya aina mbili; iko migogoro ya wao kutoboza chini kwa chini kuingia kwenye mgodi wa Tanzanite One ambao ni mgodi mkubwa kwa ajili ya kuchukua kidogo Tanzanite. Huo mgogoro tunashughulika nao.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia wachimbaji wa Mererani wana maeneo madogo, lakini hatua tuliyofikia sasa ni kuwatafutia maeneo wananchi wa Mererani ili wachimbe karibu na eneo la mgodi ule kwa sababu na kwenye kuna Tanzanite ya kutosha. Hiyo ni hatua ya pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya tatu, mgogoro ambao sana sana ni wa kiufanyakazi, ni mgogoro kati yao na waajiri wao. Mgogoro huu tunawasiliana kwa ukaribu sana na Wizara ya Kazi. Mwezi uliopita tulikaa kama Kamati na kusuluhisha mgogoro huo. Kwa sasa tunaamini kwamba wananchi wa Mererani kwa sababu watapata maeneo yao na taratibu za ajira zitazingatiwa. Kwa hiyo, matatizo sasa ya mgogoro kati yao na wachimbaji wakubwa zinakoma mara moja.

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapa maeneo ya uchimbaji wachimbaji wadogo wa Kata za Nyarugusu, Nyaruyeye na Kaseme?

Supplementary Question 3

MHE. CONSTATINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Wakati wa kampeni tulihamasisha sana vijana kujiunga kwenye SACCOS ili baadaye waweze kupatiwa maeneo ya uchimbaji wa madini. Nataka kufahamu Mheshimiwa Naibu Waziri anawaahidi nini vijana waliolundikana kwenye maeneo ya Samina, Mgusu, Nyakabale kwamba watapata lini maeneo hayo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa wananchi wa Kasema, Wanela pamoja na eneo la Geita Mjini, lakini siyo Geita Mjini tu, Nyakabale na maeneo mengine wanahitaji maeneo. Namhakikishie Mheshimwia Constantine kwamba mwaka huu tumetenga hekta 12,000 na kati ya hizo, hekta 2,000 ni maeneo ya Geita kwa hiyo wananchi wa Nyakabale, wananchi wengine wa Mtakuja na wengine ambao walikosa mgao wa Geita watapata maeneo ya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, kwa Mkoa wa Geita, mwaka 2015 na mwaka 2014, kuna SACCOS sita zilizoundwa. SACCOS mojawapo ambayo haijapata eneo la uchimbaji, ni pamoja na wakeretwa wa SACCOS ambayo ilipata lesseni tano; lakini Tupendane SACCOS walipata ekari sita pamoja na Tunakuja SACCOS walipata ekari nane; Ujamaa SACCOS kwa sababu zote zinatoka Geita walipata ekari tisa, pamoja na Mapinduzi SACCOS Kwa hiyo, wananchi wote wa Geita tunaomba wajiunge na SACCOS ili kusudi tuendelee kuwagawia maeneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Constantine sana kwamba, ningependa sana waanze kuziunda SACCOS sasa hivi, kwa sababu utaratibu sasa wa kuwatengea maeneo unaanza mwezi wa Kumi mwaka huu. Kwa hiyo, tunaomba sana SACCOS zote na siyo kwa Geita tu, ziwe tayari ili kuanzia mwezi wa Kumi waanze kugawiwa pesa. Hata hivyo, tumewatengea ruzuku sasa.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge walipitisha shilingi bilioni 6.68 kwa ajili ya ruzuku ya wachimbaji wadogo. Kwa hiyo, pamoja na kuundwa SACCOS, lakini pia tutawagawia ruzuku kwa ajili ya kuendeleza uchimbaji wao.

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapa maeneo ya uchimbaji wachimbaji wadogo wa Kata za Nyarugusu, Nyaruyeye na Kaseme?

Supplementary Question 4

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Rais alipokuja mwaka 2015 kwenye mikutano yake ya kampeni katika Jimbo la Nyang‟hwale, aliweza kuwaahidi wachimbaji wadogo wa Jimbo hilo kwamba eneo la Kasubuya litapimwa na kugawiwa wachimbaji wadogo wadogo. Je, Serikali inasemaje kwa hili kwa wachimbaji wadogo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kati ya maeneo 12 tuliyotenga kwenye Mkoa wa Geita pamoja na maeneo mengine ya Kahama ni pamoja na eneo la Kasubuya. Eneo la Kasubuya tumetenga hekta 4,098.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Hussein, wananchi wa Nyang‟hwale tayari wana eneo. Isipokuwa nawaomba sana, hata wakishindwa kupata maeneo pale Kasubuya, tunatenga maeneo mengine. Kule Chato kuna hekta 1,282. Kwa hiyo, wananchi wako bado wanaweza kwenda kule.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na maeneo yale, maeneo ya kwa Mheshimiwa wa Mbunge wa Bukombe tuna hekta 682, wanaweza wakaenda kuchimba Bukombe. Kwa hiyo, tunaendelea kutenga maeneo ili wananchi wa Kasubuya na maeneo mengine wapate maeneo ya kutosha.