Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mussa Ramadhani Sima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mjini

Primary Question

MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza: - Je, Serikali haioni haja ya kulifanya somo la kilimo kuwa la lazima kuanzia ngazi ya elimu msingi mpaka chuo kikuu kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi?

Supplementary Question 1

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Taifa letu la Tanzania linatambulika kabisa kwamba kilimo ni uti wa mgogo, na tangu uhuru tunatambulika kwamba taifa hili ni taifa la wakulima na wafanyakazi. Serikali imesema somo hili linafundishwa kwenye somo la maarifa ya jamii na stadi za kazi. Kimsingi ni mada wala si somo la kilimo ni mada zinafundishwa huko.

Mheshimiwa Spika, swali langu, swali langu, ni lini sasa...

SPIKA: Anayeuliza maswali haya ni mwalimu jamani enhee Endelea Mheshimiwa.

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, swali langu, ni lini sasa Serikali itaweka kipaumbele kuhakikisha kwamba somo hili la kilimo linafundishwa na linakuwa la lazima, kwa maana compulsory dhidi ya masomo mengine kama general study, develop and study ambayo kimsingi tija yake ni ndogo ukilinganisha na tija hii ya somo la kilimo? Serikali inasema ukienda sekondari unachagua maana yake ni option, sasa una opt nini ilhali kwenye msingi hujatengeneza somo?

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali, ikubaliane na mawazo haya kuhakikisha kwamba inalianzisha somo hili la kilimo kuanzia ngazi ya msingi mpaka chuo kikuu?

Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili, Serikali imeanza mchakato wa mabadiliko ya mtaala wa elimu, na nichukue fursa hii kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu alipoamua kwa dhati na kusema kuna haja kufanya mabadiliko ya mtaala wa elimu. Sasa swali langu hapa, ni lini Serikali itatuletea mchakato huu hapa Bungeni ili sisi tukachakata na kuhakakisha kwamba tunakuwa mstari wa mbele kuhakikisha elimu yetu hii tunaiwekea msingi ulio bora ili watoto wetu waweze kujiajiri na kuajiriwa kupitia na ujuzi huo? Ahsante sana.

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, Ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kujibu muhimu kabisa la mwalimu mwenzangu, Mwalimu Sima. Kwa kweli maswali aliyouliza ni ya msingi. Tunatambua kwamba asilimia kubwa ya wananchi wetu ni wakulima. Kwa sasa hivi, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri wangu, somo la kilimo liko kwenye sekondari kama options na kwa upande wa shule za msingi tunafanya stadi za kazi; na tunafanya mapitio ya mitaala.

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu umetuwekea semina, lakini kabla hujatutangazie ile briefing mimi nilikuwa nimepanga tarehe 6 Novemba, 2021 nifanye semina, ingawa nilikuwa sikupanga kwa Bunge lote lakini nilikuwa nimepanga nifanye na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, niwapitishe mpaka sasa hivi Serikali imefikia wapi kwenye mapitio ya mitaala, wadau wanasema kitu gani na uchaguzi wa Wizara ni nini kutokana na maoni ya wadau na mwelekeo wa Serikali kutokana na maoni ya wadau ni nini, ili sasa Waheshimiwa Wabunge wapate nafasi ya kuweza kuweka maoni yao wakati tayari maoni ya wananchi wao tumeshayaweka Pamoja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, labda niahidi tu kwamba hili nitalifanyia kazi kiutawala kuangalia kwamba tarehe 6 ambayo nilikuwa nafikiria kuwa na semina na Waheshimiwa Wabunge tayari Mheshimiwa Wangu Spika kiongozi wetu umeishaichukua hiyo tarehe kwa hiyo tutaangalia utaratibu. Ahsante sana.

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza: - Je, Serikali haioni haja ya kulifanya somo la kilimo kuwa la lazima kuanzia ngazi ya elimu msingi mpaka chuo kikuu kwa kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa uchumi?

Supplementary Question 2

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na hatua mbalimbali ambazo, tayari wameshaanza kuzichukua kwa kuona umuhimu wa kufanya mapitio ya mitaala yetu ya elimu.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nikufahamu kwa sababu kimsingi wameshafanya makongamano kadhaa ya wadau na marafiki wa elimu kwa ajili ya kukusanya maoni. Lakini wamepitia elimu ya awali, msingi na sekondari kimsingi vyuo na vyuo vikuu bado. Kwa hiyo, niulize sasa Wizara ama Serikali ina mpango gani wa kutuletea pia kufanya mapitio ya kozi ambazo zinatolewa kwenye vyuo vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, kuna maoni ya watanzania wametoa mbalimbali kuna masuala ya kilimo, kuna masuala ya ujasiriamali pamoja na stadi za kimaisha na mambo mengine mengi yote yamejadiliwa. Lakini vyuo na vyuo vikuu ambavyo ndio kimsingi vinatoa watu ambao ndio watenda kazi kwenye nchi. Ni lini sasa Serikali italeta kufanya marekebisho pia ya mtaala na masuala ya kozi ambazo zinatolewa kwenye vyuo hivyo. Ahsante. (Makofi)

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nitoe ufafanuzi na kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje. Utaratibu wa vyuo vya kati na vyuo vya elimu ya juu wana taratibu zao za kuanzisha mitaala.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano katika vyuo vikuu seneti ndio chombo kikuu ambacho kina mamlaka ya kuangalia mitaala katika vyuo vikuu na vyuo vya kati vina nyanja tofauti, vyuo vya kilimo viko chini ya Wizara ya Kilimo, vyuo vya utalii viko chini ya Wizara ya Utalii, vyuo vya afya viko chini ya Wizara ya Afya na wote wana taratibu zao. Wizara husika ndio zinakuwa na mabaraza kwa mfano Wizara ya Afya, Baraza la Madaktari ndio linaangalia mitaala ya madaktari, Baraza la Wauguzi linaangalia mitaala ya manesi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kiasi fulani hili jambo labda nilipokee kama Serikali tuangalie namna ya kuliratibu. Kwa sababu, kwa sasa hivi sio vyuo vyote vya kati vinasimamiwa moja kwa moja na Wizara ya Elimu na wala Wizara haihusiki moja kwa moja na kuidhinisha mitaala. Ila imekasimisha mamlaka kwa seneti za vyuo vikuu pamoja na vyombo ambavyo vimewekwa, kwa mujibu wa sheria katika vyuo husika kushughulika na mitaala.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu tuangalie namna gani labda kwa kuongezea kabla sijamalizia. Ni kwamba nako pia tumeelekeza wafanye mapitio ya mitaala na katika huu Mradi wa Higher Education tuna fedha ambazo tumetenga, kwa ajili ya kufanya mapitio makubwa na ndio maana mradi unaitwa mageuzi ya kiuchumi na yanajikita katika kuimarisha uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, mapitio ya mitaala yanafanyika kwa hiyo tutaangalia utaratibu mzuri wa kuratibu tupate mapitio yanayofanyika. Ili tuweze kuja kutoa taarifa kwenye chombo muhimu, ambacho ndio kinasimamia sheria na kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)