Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipandisha hadhi barabara za TARURA zinazochochea ukuaji wa uchumi kwenda TANROADS ili zipatiwe fedha za kutosha za kufanya matengenezo?

Supplementary Question 1

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa barabara ya Mwanuzi hadi Mwabuzo, kilometa 42 imekuwa ni barabara muhimu kutokana na wafanyabiashara wanaotoka Wilaya ya Meatu na Maswa kwenda Igunga kufanya biashara na hata magari ya kusafirisha pamba. Kikao cha DCC kilipeleka maombi Mkoani na RCC walishapeleka Wizarani. Je, Serikali haioni haja ya kuipandisha barabara hiyo kuwa ya TANROADS? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kipande cha Mwabuzo – Igunga, kilometa 36 kimekuwa ni cha muhimu kutokana na biashara inayofanyika hadi mabasi saba yanapita katika barabara hiyo na wakati wa masika yanalazimika kupitia Shinyanga mpaka Igunga, kilometa 300. Je, Serikali haioni haja ya kuifungua barabara hiyo kutoka Mwabuzo kilometa 36 hadi daraja la Manonga kilometa 36? (Makofi)

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba nitoe maelezo ya maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jeremiah ambayo yameulizwa kwenye Ofisi ya Rais, TAMISEMI kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja walipeleka maoni yao katika ngazi ya wilaya kama utaratibu ulivyo, yamefika kwenye ngazi ya mkoa wakajadili kwenye RCC yao na sisi Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tumeshatuma watalaam wetu katika eneo hilo, ma-engineer wameenda wametafuta tafuta taarifa mbalimbali. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute Subira, watalaamu wetu walete majibu yale, halafu kama itakidhi vigezo barabara hiyo itapandishwa hadhi na kuhudumiwa na TANROADS ili iweze kutengenezwa na ipitike wakati wote.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; barabara yake ya pili ambayo ameizungumza, tumeipokea kwa uzito tutaifanyia kazi, tuombe ushirikiano ili barabara hiyo iweze kufanyiwa matengenezo ya kudumu na wananchi wa eneo hilo waendelee kupata huduma muhimu kwa njia ya barabara. Ahsante. (Makofi)

Name

Deodatus Philip Mwanyika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipandisha hadhi barabara za TARURA zinazochochea ukuaji wa uchumi kwenda TANROADS ili zipatiwe fedha za kutosha za kufanya matengenezo?

Supplementary Question 2

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya Mtila - Lugenge mpaka Usalule ni barabara ya muhimu sana nani barabara inayounga wilaya tatu ikiunga pamoja na Hospitali kubwa ya Mkoa wa Njombe. Je, Serikali haioni kwamba ni muhimu sana hii barabara na yenyewe ikaingizwa katika mpango wa TANROADS kwa sababu mchakato umeshaanza na umekwama mahali Fulani? Ahsante.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hoja hii Mheshimiwa Mbunge amefikisha ofisini katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Kama alivyosema mwenyewe kwamba mchakato unaendelea, naomba a-speed up process hiyo na sisi tutatoa ushirikiano, itakapokidhi vigezo tutaipokea kama TANROADS, tutaitengeneza na wananchi wake watapata huduma muhimu katika eneo hilo. Ahsante.

Name

Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipandisha hadhi barabara za TARURA zinazochochea ukuaji wa uchumi kwenda TANROADS ili zipatiwe fedha za kutosha za kufanya matengenezo?

Supplementary Question 3

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. Kwa kuwa barabara ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Meatu Mheshimiwa Leah Komanya ni barabara ambayo pia inaungana na barabara ya kutoka pale Mwabuzo ikaenda Kabondo, Itinje, Mwandwitinje mpaka Mwaukoli na inaunganisha na zote hii inatoka Bariadi nyingine inatoka Meatu zinaenda zote Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Igunga.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu mapendekezo haya yote tuliyapeleka kwa pamoja kama ambavyo Naibu Waziri wa Ujenzi amejibu, sasa anaweza kunihakikishia kwamba haya maombi yote yanafanyiwa kazi kwa pamoja na muda mfupi ujenzi utaanza wa barabara hizi sasa kuwa za mkoa na baadaye ujenzi kuanza mara ili kuondoa changamoto zilizopo kwa sasa kutokana na TARURA kushindwa kumudu kukidhi mahitaji yake?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mpina, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie Bunge lako Tukufu kumwagiza Meneja wa Mkoa wa Simiyu, Shinyanga na Mwanza na maeneo yote ambayo Waheshimiwa Wabunge wameshaleta mapendekezo kwenye maeneo haya, wafanye kazi ya tathmini haraka iwezekanavyo, wawasilishe majibu Wizarani na sisi kama Serikali tuweze kuchukua hatua ili maeneo hayo yaweze kutengenezwa kwa haraka na wananchi wote waweze kupata huduma ya barabara. Ahsante. (Makofi)