Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 16 2021-11-03

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipandisha hadhi barabara za TARURA zinazochochea ukuaji wa uchumi kwenda TANROADS ili zipatiwe fedha za kutosha za kufanya matengenezo?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, naomba kutoa maelezo mafupi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kupandisha hadhi barabara ni la kisheria kwa kuzingatia vigezo vilivyowekwa. Barabara ambayo inakidhi vigezo kutoka daraja la barabara ya wilaya kwenda daraja la barabara ya mkoa inatakiwa ijadiliwe kwenye kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa husika. Ikionekana inakidhi vigezo ndio Bodi hiyo kupitia Mwenyekiti wake itamshauri Waziri mwenye dhamana na barabara kuwa barabara husika imekidhi vigezo vya kuwa na hadhi ya Barabara ya Mkoa na hivyo ipandishwe daraja na kuwa Barabara ya Mkoa chini ya TANROADS.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la uwezo wa TARURA hususani uwezo wa rasilimali fedha, Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo, itaendelea kuiwezesha TARURA kwa kuiongezea fedha na kuijengea uwezo ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na weledi.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza azma hiyo, katika mwaka wa fedha 2021/2022 zimetengwa shilingi bilioni 966.90 ikilinganishwa na shilingi bilioni 275.03 zilizotengwa mwaka wa 2020/2021 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara na madaraja zinazosimamiwa na TARURA.