Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: - Je, ni lini akina Mama zaidi ya 300 waliokuwa Wafanyakazi wa Kiwanda cha Kiliflora Wilayani Meru watalipwa stahiki zao baada ya Kiwanda hicho kufungwa?

Supplementary Question 1

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, sijaridhika na majibu yake. Kwa taarifa rasmi zilizopo ni kwamba, viwanda hivi pamoja na mashamba viko chini ya Msajili wa Hazina. Msajili wa Hazina pamoja na Wizara ya Fedha ndiyo wanaotakiwa kuwalipa wafanyakazi hawa.

Mheshimiwa Spika, naomba kusikia commitment ya Serikali. Je, ni lini wafanyakazi hawa 502 watalipwa na Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Viwanda hivi vinaenda sambamba na mashamba yale maua na mbogamboga. Mashamba haya na viwanda ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Mkoa wa Arusha pamoja na sekta hii ya maua na mbogamboga.

Naomba kujua Serikali ina mikakati gani wa kuyafufua mashamba haya? Ahsante. (Makofi)

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, napenda kuongezea majibu mazuri ambayo amejibiwa na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, siyo sahihi kwamba Serikali ndiyo inapaswa kulipa madeni haya, kwa sababu kama ambavyo ameeleza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda kwamba TIB ilipewa dhamana ya kuhakikisha kwamba inarudisha fedha ambazo Kiliflora ilikuwa imekopeshwa. Fedha hii ilirudishwa kupitia mnada ambapo Serikali ilinunua mashamba yale kihalali, lakini hawa ambao wanadai wanadai vitu viwili vikubwa: Kwanza wanadai malimbikizo ya mishahara kwa kampuni ambayo ilikuwa imewaajiri pamoja na mafao.

Mheshimiwa Spika, haya ni madai ambayo yanapaswa kulipwa na mwajiri ndiyo maana hata katika kesi waliyofungua walimshitaki muajiri na Mahakama kupitia Tume ya Usuluhishi wakatoa maamuzi kwamba, hii kampuni iwalipe kwa hiyo, maamuzi tayari yalishatoka kwamba, kampuni hii ndiyo inapaswa kuwalipa hawa wadai.

Mheshimiwa Spika, nawashauri hawa wadai kwamba pengine wangeweza kuwasiliana na vyombo vya dola ili waweze kuwasaidia kuwatafuta hawa wanaowadai waweze kuwalipa mali yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na namna ambavyo mashamba haya yataendelezwa kwa sababu, mashamba haya sasa hivi yapo tayari kwa Serikali, kuna mikakati mikubwa ya kuhakikisha kwamba tunaimarisha sekta ya kilimo kupitia rasilimali mbalimbali ambazo zinamilikiwa na Serikali, yakiwepo mashamba haya, lakini kwa kuwa, sasa hivi muda ni mfupi siwezi kueleza mikakati hiyo ambayo iko chini ya benki ya TIB kwa kirefu.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Mheshimiwa Mbunge nitakupatia baadae. (Makofi)