Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Seif Khamis Said Gulamali

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manonga

Primary Question

MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa majosho katika Wilaya ya Igunga, hususan Jimbo la Manonga?

Supplementary Question 1

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Wilaya ya Igunga ni wilaya moja wapo inayoongoza kwa mifugo mingi sana hapa Tanzania, je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza idadi ya majosho, hasa Jimbo la Manonga, kutoka majosho matatu hata angalau kufika majosho kumi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika siku 100 za Mheshimiwa Rais, mama Samia Hassan Suluhu, tumemuona akikutana na Mwanamfalme wa Saudi Arabia na wamejadili juu ya masuala ya mifugo, hasa kuuza mifugo lakini pia kuuza nyama nje ya nchi. Je, Wizara imejipangaje kutumia fursa hii; mkakati wake ni upi? Ahsante. (Makofi)

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Manonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni kuongeza idadi ya majosho katika Jimbo la Manonga. Naomba tu nipokee ombi hili la Mheshimiwa Mbunge na nimuahidi kwamba Wizara italifanyia kazi kwa kusudi la kuongeza idadi ya majosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni hili la mkakati wa Serikali juu ya kuongeza biashara ya nyama na mifugo nje ya nchi. Kwanza nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan; katika siku hizi 100 moja ya Wizara ambazo amezifanyia kazi kubwa ni hii Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi. Naomba tu nimhakikishie
Mheshimiwa Mbunge ya kwamba Wizara imejipanga vyema kuhakikisha kwamba fursa hii ya kuuza nyama na mifugo nje inatumika na inatumika ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja, ni kwa kupunguza kodi mbalimbali ambazo zilikuwa ni kikwazo. Lakini pili, ni kuendelea kushirikiana vyema na sekta binafsi ili kuweza kushamirisha biashara ya mifugo. Na mwisho, mkakati wetu wa kopa ng’ombe lipa ng’ombe, kopa mbuzi lipa mbuzi, tutaupa kipaumbele sana ili kuongeza uzalishaji katika nchi. Ahsante sana.