Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: - Je, ni lini makubaliano ya kibiashara yatafanyika baina ya taasisi za Umma na makampuni binafsi yanayolima kahawa Mkoani Kilimanjaro ili kuzalisha miche bora yenye ukinzani dhidi ya magonjwa na kuigawa kwa wakulima bila malipo?

Supplementary Question 1

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini niseme wazi kwamba ninapotamka zao la kahawa aina ya Arabic katika Mkoa wa Kilimanjaro ni zao dume, ni zao ambalo linawapatia wanaume kipato. Wakati zao hili linapauka, wanaume wote sasa wanakwenda kuwabana akina mama kwenye zao lao la migomba, kwenye zao lao la mbogamboga, maharage na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, katika swali la msingi niliomba kuelezwa ni nini makubaliano ya kibiashara kati ya Serikali na wafanyabiashara wenye estates? Kwa sababu wale ndio wenye mashamba makubwa ya kahawa yanayozunguka wakulima wadogowadogo, estates hizo zikiwemo Tchibo, Machare, Kikafu na kadhalika.

Sasa ni lini Serikali itakubaliana na wakulima hao wa ma-estate wawasaidie hawa wakulima wadogo wadogo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; sina tatizo wala shida kabisa na uzalishaji wa miche kutoka TaCRI, lakini TaCRI ni kituo kimojawapo tu kinachozalisha miche pamoja na hiyo mingine aliyosema Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, je, Naibu Waziri yuko tayari sasa kufuatana na mimi mama yake, mguu kwa mguu twende katika mashamba ya wananchi tuone ambavyo zao hilo limepauka?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mama Shally Raymond kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, suala la kufuatana na Mheshimiwa Mama Shally kwenda Mkoa wa Kilimanjaro, nimhakikishie niko tayari na tutapanga mimi na yeye kwa sababu nina wajibu kwake, ni mama yangu, kanilea miaka mitano nikiwa next kwake. Kwa hiyo, nitakwenda na nitazunguka naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuingia mikataba na estates, kwanza mikataba ni willingness kati ya mtoa huduma na anayeombwa kutoa huduma, kwa hiyo, sisi kama Serikali pale ambapo watu wako tayari kuingia mikataba na Taasisi yetu ya TaCRI kwa gharama nafuu ambayo siku ya mwisho haitaweza kumuumiza mkulima na conditions ambazo haziwezi kutuumiza, tuko tayari.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi tuna programu kubwa ya kuzalisha zaidi ya miche milioni 20 ya kahawa ambayo tutaigawa katika kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa hiyo, kwa wafanyabiashara ambao wako tayari kuingia kwa conditions ambazo ziko wazi na TaCRI, sisi wala hatuna tatizo juu ya hilo na ndiyo maana tumetaja baadhi ya taasisi ambazo tumeshaingia nazo makubaliano na baadhi ya wakulima ambao tutaingia nao makubaliano. Lakini tukienda pamoja kama tutakutana na hao wenye estates kubwa tutajadiliana namna ya kufanya.

Name

Agnes Elias Hokororo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: - Je, ni lini makubaliano ya kibiashara yatafanyika baina ya taasisi za Umma na makampuni binafsi yanayolima kahawa Mkoani Kilimanjaro ili kuzalisha miche bora yenye ukinzani dhidi ya magonjwa na kuigawa kwa wakulima bila malipo?

Supplementary Question 2

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, lakini uzalishaji wa miche ya kahawa unafanana na uzalishaji wa miche ya mikorosho iliyopo Mkoani Mtwara. Vikundi vinavyozalisha miche ya korosho Mkoani Mtwara vinaidai Serikali tangu mwaka 2018 na hivi karibuni tulipata kauli ya Serikali kwamba hundi imeandikwa.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni je, ni lini Serikali italipa vikundi hivyo vya uzalishaji wa miche ya korosho vilivyoko Mkoani Mtwara?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, nitumie Bunge lako kuwaambia kwamba wakulima wadogo wote ambao walikuwa wanadai zaidi ya shilingi bilioni 1.8, tayari fedha hizi zimeshatoka na sasa tunafanya utaratibu ili Wizara ziweze kupelekwa Bodi ya Korosho na Bodi ya Korosho ianze kulipa wakulima. Anytime kuanzia sasa fedha hizo watakuwa wameanza kuzipata.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie tu kwamba kwa sababu utaratibu tuliokuwa tumejiwekea na ninashukuru Waziri wa Fedha hapa alisema kwamba taasisi yoyote ya Serikali itakayopokea fedha dakika za mwisho, hakutakuwa na ule utaratibu wa kuzirudisha, tunaamini kwamba kati ya wiki ijayo mpaka mwanzoni mwa mwezi Julai fedha hizi zitanza kulipwa kwa sababu tayari utaratibu wake umeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, vilevile watumishi wa umma walioingia mikataba na Bodi ya Korosho, malipo yao na yenyewe kama Wizara sisi tumesha-compile na kuzipeleka Wizara ya Fedha ili na wao waweze kupata haki yao kwa sababu kuwa watumishi wa umma hakuwaondolei haki ya kulipwa kama ambavyo walitakiwa kulipwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kuwasiliana kwa karibu kuhakikisha kwamba mpaka Julai wakulima wote fedha zao wawe wameshazipata kwa sababu fedha hizo hata zikiingia kwetu tarehe 30 hazitarudi Hazina.

Name

Dr. Oscar Ishengoma Kikoyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba kusini

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: - Je, ni lini makubaliano ya kibiashara yatafanyika baina ya taasisi za Umma na makampuni binafsi yanayolima kahawa Mkoani Kilimanjaro ili kuzalisha miche bora yenye ukinzani dhidi ya magonjwa na kuigawa kwa wakulima bila malipo?

Supplementary Question 3

MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, matatizo ya zao la kahawa ya Mkoa wa Kilimanjaro yanafanana sana na matatizo ya kahawa ya Mkoa wa Kagera. Mavuno ya kahawa katika Mkoa wa Kagera huanza mwezi Aprili hadi Mei, lakini mpaka juzi Vyama vya Msingi vilikuwa havijafungua msimu wa kahawa.

Mheshimiwa Spika, na tatizo kubwa lililopo hasa Wilaya ya Muleba, wananchi wanabugudhiwa na task force ambayo imeundwa ambayo inajumuisha watu wa PCCB, Usalama wa Taifa na watu wa Kilimo. Kila anayekutana naye anatoka shambani ana gunia moja anakamatwa na kupelekwa kituo cha polisi.

Naomba kauli ya Serikali, je, ni nini kauli ya Serikali kukomesha vitendo viovu hivi ambavyo vinawabugudhi wakulima kwa kisingizo kwamba wanalangua kahawa ilhali wako kwenye Wilaya yao, wako kwenye tarafa yao na vijiji vyao? (Makofi)

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Muleba Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, niseme na nirudie tena, tumefanya vikao na viongozi wa Mkoa wa Kagera, tumefanya vikao na vyama vikuu vya ushirika vya Kagera, tumefanya vikao na wanunuzi binafsi; la kwanza, hatumzuii mkulima yeyote kupitia chama chake cha msingi kuuza mazao yake kwa mfanyabiashara katika level ya chama cha msingi. Hili ni jambo la kwanza, na tumeruhusu na tumetoa leseni. Na msimu umeshafunguliwa. Na wiki iliyopita tulikuwa na mkutano hapa Dodoma wa wadau wote wa kahawa.

Mheshimiwa Spika, la pili, tuwaombe viongozi katika ngazi za Halmashauri na Wilaya. Sekta ya kilimo haiwezi kusimamiwa kimabavu, sekta ya kilimo inasimamiwa kwa misingi ya win-win. Mkulima anayevuna mazao yake kutoka shambani kuyapeleka kwenye nyumba yake ama kuyapeleka kwenye chama chake cha msingi, naomba kupitia Bunge lako niwaombe viongozi walioko katika Halmashauri na Wilaya wasiwabughudhi.

Mheshimiwa Spika, lakini haturuhusu vilevile wafanyabiashara wanaowafuata wakulima mashambani kwenda kununua mazao chini ya bei ya soko, halafu wao kupeleka kwenye minada na Chama cha Msingi ili waweze ku-benefit na bei. Hilo hatutaruhusu na wala hatutaruhusu mfanyabiashara yeyote anayechepusha mazao kuvusha kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda.

Mheshimiwa Spika, tunawataka na nitumie Bunge lako kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, kama mna wanunuzi kutoka Uganda ambao wana uwezo wa kutupa bei nzuri, waleteni Wizarani tutawapa leseni, watakwenda kununua katika mfumo rasmi bila kubugudhiwa na mtu yeyote.