Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 59 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 496 2021-06-25

Name

Shally Josepha Raymond

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SHALLY J. RAYMOND aliuliza: -

Je, ni lini makubaliano ya kibiashara yatafanyika baina ya taasisi za Umma na makampuni binafsi yanayolima kahawa Mkoani Kilimanjaro ili kuzalisha miche bora yenye ukinzani dhidi ya magonjwa na kuigawa kwa wakulima bila malipo?

Name

Hussein Mohamed Bashe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shally Josepha Raymond, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uzalishaji wa miche bora ya kahawa hufanyika kupitia wakulima binafsi, vikundi vya wakulima, Vyama vya Ushirika, Taasisi ya Utafiti ya TaCRI na mikataba baina ya TaCRI na kampuni binafsi au shirika.

Mheshimiwa Spika, kutokana na gharama kubwa ya uzalishaji wa miche hususani pale ambapo hakuna ufadhili maalum wa taasisi au shirika, kumekuwepo na utaratibu wa wakulima kuchangia gharama kidogo ili kuwa na uzalishaji endelevu na upatikanaji wa miche bora.

Mheshimiwa Spika, mathalani wakulima hutakiwa kuchangia kiasi cha shilingi 100 kwa kila mche sawa na asilimia 10 ya gharama halisi ya mche. Kati ya Julai, 2016 mpaka 2021 TaCRI imezalisha jumla ya miche 2,308,606 ambayo imeendelea kusambazwa Mkoani Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, TaCRI imekuwa ikiingia mikataba ya kuzalisha miche bora yenye ukinzani dhidi ya magonjwa na kuisambaza kwa wakulima kadri ya mahitaji. Mikataba hiyo ni pamoja na uzalishaji wa miche 100,000 uliofanyika kati ya mwaka 2018 na 2019 ambapo TaCRI ilishirikiana na Ushiri AMCOS ya Wilayani Rombo kuzalisha miche hiyo.

Mheshimiwa Spika, TaCRI kati ya mwaka 2016 na 2019 ilishirikiana na Taasisi za Hivos na Solidaridad kutoa mafunzo kwa wazalishaji wa miche bora ya kahawa ambapo jumla ya miche 890,677 ilizalishwa na kusambazwa kwa wakulima katika Wilaya za Same, Mwanga na Moshi.