Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Primary Question

MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaanza kujenga na kukarabati majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Mbinga kutokana na kukosa baadhi ya majengo na yaliyopo kuchakaa?

Supplementary Question 1

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru Naibu Waziri wa TAMISEMI kwa majibu mazuri, lakini vile vile niipongeze Serikali kwa kutoa huduma nzuri katika maeneo mbalimbali kwenye fani ya afya. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa hospitali hiyo ilijengwa mwaka 1970, jengo la OPD na jengo la upasuaji ni majengo ambayo yamepitwa na wakati na hayaendani na hadhi ya hospitali ya wilaya pamoja na jengo la wodi ya watoto ambao limekosekana kabisa.

Je, Serikali itaanza lini kushughulikia ujenzi wa majengo ya OPD, upasuaji na wodi ya Watoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika hospitali hiyo kuna uhaba wa watendaji, wafanyakazi, Madaktari na watendaji wasaidizi. Je, ni lini Serikali itachukua hatua ya kuhakikisha kwamba changamoto hiyo inatatuliwa? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas William, Mbunge wa Mbinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee pongezi za Mheshimiwa Mbunda na kwamba Serikali imeendelea kuboresha sana huduma za afya kwa kujenga miundombinu, lakini pia kuhakikisha vifaatiba na dawa zinapatikana. Kuhusiana na hospitali hii kuwa kongwe ni kweli. Hospitali hii imejengwa miaka ya 70 na ni hospitali ambayo kimsingi ni chakavu, inahitaji kuboreshewa miundombinu ili iweze kuendana na majengo ambayo yanaweza kutoa huduma bora za afya kwa ngazi ya hospitali ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hayo, ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba Serikali imeanza kufanya tathmini ya uchakavu wa majengo yale na upungufu wa majengo ambayo yanahitajika katika hospitali ile ili sasa tuweze kuona namna ya kutenga fedha kwa ajili ya kuanza either, kukarabati majengo yale na kuongeza yale majengo yanayopungua au kuanza ujenzi wa hospitali mpya. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tathmini hiyo itakapokamilika tutakuja na jawabu la njia sahihi ya kwenda kutekeleza ili kuondokana na changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kuna changamoto ya upungufu wa watumishi katika kada mbalimbali katika hospitali hiyo na nchini kote kwa ujumla. Katika bajeti yetu tumeeleza mipango kwamba baada ya kukamilisha miundombinu ya majengo, tutakwenda kuhakikisha tunaboresha upatikanaji wa vifaatiba, lakini suala linalofuata muhimu na linapewa kipaumbele cha hali ya juu ni kuhakikisha sasa tunakwenda kuomba vibali vya kuajiri watumishi wa afya katika ngazi zote za vituo vya afya, zahanati na hospitali ili tuweze kutoa huduma bora zaidi. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunda kwamba, katika Hospitali hii ya Mji wa Mbinga pia tutaweka kipaumbele katika kuajiri watumishi ili kuendelea kuboresha huduma za afya.