Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 14 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 114 2021-04-21

Name

Jonas William Mbunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Primary Question

MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga na kukarabati majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Mbinga kutokana na kukosa baadhi ya majengo na yaliyopo kuchakaa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga ina majengo saba ambayo ni jengo la akinamama, jengo la huduma za Bima, jengo la upasuaji, jengo la maabara, jengo la kuhifadhia maiti, jengo la mionzi na jengo la wagonjwa wa nje. Baadhi ya majengo hayo yana uchakavu wa wastani na mengine yana uchakavu wa hali ya juu. Jengo muhimu linalokosekana katika hospitali hiyo ni jengo la wodi ya watoto. Serikali imefanya tathmini ya hali ya uchakavu wa miundombinu ya hospitali hiyo ili kuona namna bora ya kufanya ukarabati au ujenzi wa hospitali mpya ya halmashauri. Kuanzia Mwaka wa Fedha 2017/2018 hadi 2019/2020, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri imefanya ukarabati wa jengo la wodi maalum na jengo la wagonjwa wa nje kwa gharama ya shilingi milioni 45.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga na katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imeipatia Halmashauri ya Mji wa Mbinga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya, Kalembo ambacho ukarabati wake umekamilika na huduma zinatolewa ikiwemo huduma za upasuaji. Aidha, mwaka 2021 Serikali imeipatia shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya Zahanati za Kagugu, Iringa na Ruwaita. Vile vile katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imeomba kuidhinishiwa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa awamu itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za afya nchini kote ikiwemo katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga.