Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kuruhusu wananchi wanaoishi kwenye Miji ambayo ipo kando ya barabara kuu kama Mji wa Mafinga kufanya biashara kwa saa ishirini na nne?

Supplementary Question 1

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Leo tutajadili hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na sehemu ya hotuba hiyo tutajadili suala la ajira hususan kwa vijana. Nina maswali mawili ya nyongeza kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali iliruhusu tusafirishe mazao ya misitu kwa saa 24 na hivyo kusisimua na kuchechemua uchumi sio wa Mafinga tu na maeneo mengine. Je, Serikali iko tayari kufanya upendeleo maalum kwa Mji wa Mafinga kutokana na nature yake ya kibiashara kuruhusu baadhi ya maeneo watu kufanya biashara saa 24 na yenyewe ikabaki na suala la ulinzi ambayo ni kazi kuu ya Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali pili, katika jibu la msingi Serikali imesema kuna changamoto ya miundombinu muhimu kama vile taa, kamera na kadhalika. Sisi kama Halmashauri tuko tayari kujenga baadhi ya miundombinu lakini je, Serikali iko tayari kutusaidia japo taa za barabara katika maeneo muhimu katika njia panda za Itimbo, Madibila, Mufindi na Sokoni ili kuwawezesha wananchi hawa kuendelea kujiajiri na kujipatia kipato na hivyo kuwa na mchango katika Serikali na mifuko yao?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Mheshimiwa Mbunge alikuwa anataka upendeleo maalum kwa Mji wa Mafinga ili uweze kufunguliwa. Katika jibu langu msingi nilieleza kabisa moja ya jukumu kubwa la Serikali ambalo tunalifanya sasa ni kuhakikisha tunajenga miundombinu na usalama unakuwepo. Baada ya kutathmini ndipo tunaweza kuruhusu Mji wa Mafinga ili uweze kufanya biashara kwa saa 24.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo ni la msingi kabisa Mheshimiwa Mbunge ameainisha commitment ya Halmashauri yake kwamba wao kama Mafinga Mji wako tayari kujenga baadhi ya miundombinu muhimu na sisi kama Serikali tuweze kusaidia katika kuweka hizo taa za barabarani. Nafikiri wazo hilo ni jema na mimi niungane kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kusema kwamba tunaomba Halmashauri ya Mji Mafinga waanze hiyo hatua ya kutengeneza hiyo miundombinu muhimu na sisi tutatuma wataalam wetu waende kufanya tathmini, ili tuweze kuwaruhusu waweze kufanya hiyo biashara yao kwa saa 24 na sisi tutawasaidia katika hiyo sehemu itakayobakia.