Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Asha Abdullah Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA Aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaendeleza kimasomo watoto wa kike waliokatisha masomo kwa kupata ujauzito?

Supplementary Question 1

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni zito linalowakuta wasichana wetu hawa, linavuruga maisha yao utaratibu wao na kuleta simanzi na huzuni katika familia japokuwa kaja kiumbe lakini kaja vipi na atahudumiwa namna gani. Je, Serikali haioni kwamba ni wakati muafaka wa kuwarudisha wasichana hawa wakaendelea na masomo yao baada ya kujifungua kuliko kuwapeleka kwenye vituo nje ya mfumo rasmi. Kwa kuwa mimba siyo maradhi ya kuambukiza wao walikuwa wakazane kuleta mitaala juu ya ngono, uzazi. (Makofi)

Swali la pili Je, Serikali haioni kwamba kuzuia watoto wa kike waliopata mimba kuendelea na masomo yao na kuwaachia watoto wa kiume waliohusika kuendelea kama vile hawajafanya chochote siyo ubaguzi wa kijinsia?(Makofi)

Mheshimiwa Spika, waliofanya makosa watu wawili, bakora anapigwa mtu mmoja kweli hiyo ni haki? (Makofi)

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri amelizungumza ni kweli tumeweka huo utaratibu na kama unakumbuka kupitia mradi wetu wa SEQUIP ambao karibu tunaanza kuutekeleza tumeweka pia kipengele cha kuangalia Watoto wanaopata ujazito wakiwa shuleni na tutaenda kuimarisha vituo vyao ambavyo tumevieleza katika jibu la msingi.

Mheshimiwa Spika, jambo hili limekuwa linazungumzwa kwa muda mrefu na kwa sababu sasa ndiyo tunaanza kutekeleza mpango mahsusi ambao tumeuweka ningeomba tutekeleze angalau kwa kipindi cha mwaka huku Serikali ikiendelea kutafakari maoni ambayo yamekuwa yanatolewa na wadau ili tuone namna bora zaidi ya kutekeleza hayo maoni ambayo yamekuwa yakitolewa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili kwamba kwanini anayehusika asichukuliwe hatua. Utakumbuka kwamba mwaka 2016 Bunge lako Tukufu lilitunga sheria ambayo inatoa adhabu kali kwa mtu yeyote ambaye anajihusisha na masuala ya mapenzi shuleni kwa wanafunzi au mtu ambaye anakatiza ndoto ya watoto wa kike ya kupata elimu. Yeyote ambaye anabainika kwa mujibu wa sheria hiyo iliyotungwa mwaka 2016 anapata adhabu ya kifungo cha miaka 30. Nashukuru kwa nafasi.