Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zuena Athumani Bushiri

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZUENA A. BUSHIRI Aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza umeme katika Vijiji na Vitongoji kupitia REA III hasa katika maeneo ambayo nguzo zimetelekezwa barabarani zaidi ya miaka miwili?

Supplementary Question 1

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu ya mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto ya miradi kutokukamilika kwa wakati. Nini kauli ya Serikali kwa wakandarasi ambao hawamalizi miradi yao kwa wakati na kuchelewesha huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili kumekuwa na wimbi kubwa sana la wizi wa miundombinu ya umeme, mfano kule Moshi Manispaa, katika Kata za Soweto, Boma Ng’ombe, Barabara ya Bonite pamekuwa na wimbi la vijana ambao wanaiba miundombinu hii. Je, Serikali hii inachukua hatua gani kudhibiti uharibifu huu? Ahsante. (Makofi)

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali kuhusiana na miradi ambayo haijakamilika ni kwamba, kwanza ifikapo Disemba mwaka huu 2021 miradi yote ambayo siyo ya REA III round II itakuwa imekamilika kwa maana ya REA II na REA III round I itakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na changamoto kidogo zilizopelekea miradi hii kuchelewa, sababu mojawapo ikiwa ni kwamba ni vile vifaa ambavyo vilikuwa vinaagizwa nje ya nchi vilichelewa kufika kwa sababu ya lockdown za wenzetu kule kushindwa kuleta vile vifaa kwa wakati. Shida nyingine ilikuwa ni maeneo mengine miundombinu kuharibiwa na mvua kali na hivyo watu wakashindwa kukamilisha kazi zao kwa wakati. Hata hivyo, tumejiwekea utaratibu na tunawaahidi Watanzania kwamba ifikapo Disemba mwaka huu hakutakuwa kuna mradi wowote wa REA III round I au REA II ambayo inaendelea, itakuwa yote imekwisha. Miradi ambayo itakayokuwa inaendelea ni ya REA III round II ambayo nayo Disemba mwakani itakamilika.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha mambo haya hayajitokezi tena, Serikali ilielekeza kwamba vifaa vyote vipatikane hapa nchini na kweli vinapatikana. Hiyo inatuongezea speed ya kufanya kazi hizi na kuzimaliza mapema.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Serikali imelifanya ni kuhakikisha sasa inatoka kwenye kufanya kazi hizi kwa mtindo wa goods na kuziweka kwenye works, kwamba mtu atalipwa baada kukamilisha kipande fulani cha kazi ambacho anatakiwa kukifanya na hiyo inatusaidia kusimamia vizuri maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo Serikali imelifanya, tumehakikisha sasa tunakwenda kila kanda na kila mkoa kuweka msimamizi wa miradi yetu ya REA, akae kule masaa 24 akimsimamia mkandarasi anayefanya kazi kuhakikisha kwamba kazi inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne, tumehakikisha kwamba, wale wakandarasi wanaokwenda kwenye maeneo yetu tumewakabidhi kwa Waheshimiwa Wabunge ili na wenyewe wawe wasimamizi namba moja wa kuhakikisha kila siku wanawaona site na pale ambapo panatokea hitilafu ya kuwa mzembe mzembe, basi taarifa hizo zinatufikia mara moja. Tunaamini njia hizo zitatusaidia.

Mheshimiwa Spika kwenye jambo la pili; jambo la wizi siyo la mtu mmoja kulikemea, tunawaomba wenzetu tuendelee kushirikiana, sisi kama Wizara tunawapa support kubwa sana wakandarasi wanapotoa taarifa za kuibiwa, tunasaidiana nao moja kwa moja kuhakikisha kwamba tunafuatilia, kuhakikisha tunawachukulia hatua wale walioiba miundombinu. Pia tunaweka mikakati mingine ya ziada ya kuwasaidia wale wakandarasi kuweka vifaa vyao katika godown za TANESCO ili angalau viwe katika usalama zaidi.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumewaelekeza, wao ndiyo wenye wajibu wa kuhakikisha mali hizo haziibiwi ili wafikishe mizigo ile na kazi ifanyike kwa wakati. Tunaamini kufikia Disemba mwakani, jambo la kupeleka umeme REA III round II litakamilika kwa muda uliopangwa kwa mujibu maelekezo ya Serikali. Nashukuru.