Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Issa Jumanne Mtemvu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibamba

Primary Question

MHE. ISSA J. MTEMVU Aliuliza:- (a) Je, ni lini Serikali itatekeleza kikamilifu Waraka Na. 3 wa mwaka 2015 kuhusu Muundo wa Kada ya Uhasibu na Ukaguzi wa Ndani? (b) Je, ni lini Kitengo cha Uhasibu na Fedha katika Wizara na Sekretarieti za Mikoa zitapewa hadhi ya kuwa Idara?

Supplementary Question 1

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali ya kuridhisha kwa kiasi, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, pamekuwa na watumishi wengi ambao wamekaa muda mrefu, zaidi ya miaka kumi hadi ishirini wakiwa wanalilia suala la muundo huu ambapo umetoka Waraka Na.3 wa Mwaka 2015 bila kutekelezwa kwa wakati. Serikali ina mpango gani wa kupandisha vyeo vyao kwa mserereko ili kuzingatia muda waliotumia kazini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, suala la hadhi ya Kitengo cha Uhasibu, ni kweli Serikali inajibu juu ya vigezo ambavyo vinafanyiwa tathmini mara kwa mara na Ofisi ya Rais, Utumishi. Natambua vigezo vyenyewe vinazingatia job analysis na job design. Kwa msingi huo, ni ukweli kada hii imeacha kutumia local standards kwa muda mrefu sana na sasa wanatumia international standards katika kutengeneza mizania mbalimbali ya taasisi. Vilevile hata ripoti za CAG tunaziona jinsi gani zinavyotoka tayari kila mmoja anahamaki juu ya kuiona hadhi ya taasisi inabebwa na sehemu au kitengo hiki. Tunao mfano, juzi tu taarifa ya CAG baada ya kuitoa tayari viongozi wa Serikali wametoa maelekezo magumu kwa section hii, yaani Wakuu wa Idara au Vitengo hivi.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho hadhi hii inategemea kazi kubwa wanayoifanya. Tayari uchumi na mipango wana hadhi ya Kurugenzi…

SPIKA: Mimi nilifikiri swali huwa linakuwa ni swali.

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, ni swali, natengeneza hoja ya kuuliza swali la mwisho hili.

SPIKA: Hapana, unahutubia Mheshimiwa.

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, basi kwa misingi hiyo miwili sasa Serikali haioni ni muda mwafaka wakifanya analysis yao wa kukipa hadhi Kitengo hiki cha Uhasibu na Idara ya Ukaguzi?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza; kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mtemvu kwa kuwatetea watumishi hawa, lakini nimjulishe kwamba ni dhamira ya Serkali na Serikali imekuwa ikifanya hivyo kila mwaka kuhakikisha kwamba inapandisha vyeo na hadhi za wafanyakazi na watumishi wake ambao wanafanya kazi vizuri. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba hao Wakaguzi wa Hesabu, Wahasibu pamoja na Wasaidizi wao watapandishwa vyeo pale ambapo hali ya bajeti itaruhusu lakini kwa kuzingatia vigezo ambavyo vimewekwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusiana na vigezo hivyo, kama ambavyo nimejibu katika swali lake la msingi ni kwamba utaratibu huu ambao umewekwa upo kwa mujibu wa Sheria ile ya Bodi ya Wahasibu na Wakaguzi ambayo ndiyo imesababisha kutayarishwa Waraka huu Na.3. Kwa kuzingatia sheria hiyo na Waraka ule, ndiyo utaratibu huohuo ambao utaendelea kama ambavyo nimejibu katika swali la msingi.