Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. KUNTI Y. MAJALA Aliuliza: - Je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa kike katika Shule za Msingi Birise na Donsee ambazo hazina walimu wa kike?

Supplementary Question 1

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi tena ya kuweza kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Wilaya ya Chemba tuna upungufu wa walimu wa kike chini ya asilimia 50. Huyu mwalimu ambaye amepelekwa Shule ya Msingi Donsee ametolewa kwenye shule nyingine, wamemhamisha kutoka shule hiyo wamempeleka shule nyingine, lakini nataka kwenye mpango wa Serikali nimeambiwa hapa Serikali iko kwenye mpango.

Ni lini Serikali itatuletea walimu wa kike kwa ajili ya kunusuru maisha ya watoto wetu wa kike?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, changamoto zinazosababisha walimu wetu wa kike wasikae kwenye shule zetu hizo ni ukosefu wa nyumba za walimu, miundombinu ya barabara, ukosefu wa umeme, kuna changamoto nyingi kadha wa kadha. Walimu wakifika kule kwa mfano Shule ya Msingi Birise iko umbali wa zaidi ya kilometa 160, bodaboda ni shilingi 45,000 mwalimu wa kike unampeleka pale, hawezi kukaa mazingira ni magumu. Hata zahanati tu hawana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza Serikali, ni lini itakwenda kujenga nyumba za walimu, kuboresha miundombinu ya barabara, lakini pia suala zima la umeme ili tunapopeleka walimu wetu wa kike waende wakakutane na mazingira rafiki wapate kuishi kule na hatimaye watoto wetu wa kike waweze kupata na wao fursa ya kuhudumiwa na walimu hawa wa kike? Nakushukuru.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba nitumie fursa hii kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameuliza lini Serikali itapeleka walimu wa kike katika Halmashauri ya Chemba? Kama ambavyo nilijibu katika swali langu la msingi, Serikali bado imeendelea na utaratibu wake wa kawaida wa kuajiri walimu mara kwa mara na bahati nzuri sasa hivi tuko katika mpango wa mwisho wa kutoa ajira mpya kwa walimu kwa hiyo, hilo suala lake tutalizingatia na tutaangalia zaidi jinsia, ili kuhakikisha kwamba, tunawasaidia watoto wa kike katika shule zote nchini.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili, alikuwa anauliza moja ya changamoto kubwa ni ukosefu wa miundombinu, hususan nyumba za walimu, na ndio sababu ambayo imesababisha walimu wengi kutokufika katika baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali inatambua kwamba changamoto hiyo ipo na katika moja ya mkakati wa Serikali ambao umekuwepo sasa hivi, Serikali ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, imekuwa ikijenga miradi mingi kwa maana ya miundombinu katika sekta ya elimu. Tumekuwa tukijenga mabweni, madarasa, mabwalo, miundombinu ya vyoo pamoja na nyumba za walimu za two in one.

Mheshimiwa Spika, sasa lini tutajenga, mimi niseme tu kwamba, kwa sababu tuna mpango mwingine wa tatu ambao tutaueleza katika bajeti na kwa sababu umeelezeka huko ndani kulingana na bajeti, tutapeleka hizo nyumba za walimu katika yale maeneo ambayo yana shida zaidi ili kuhakikisha kwamba walimu wa kike wanafika maeneo hayo. Ahsante sana. (Makofi)