Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza: - Serikali imeanzisha Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla Wilayani Urambo: - (a) Je, ni lini Serikali itatoa elimu elekezi kwa wananchi wa maeneo hayo juu ya matumizi ya eneo husika baada ya mabadiliko yaliyotokea? (b) Kutokana na ongezeko la watu, je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi maeneo kwa ajili ya ufugaji nyuki, mifugo na kilimo?

Supplementary Question 1

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu maswali vizuri kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini napenda Serikali itambue kwamba wananchi wa Urambo wanashukuru kupata hifadhi lakini kwa kuwa kulikuwa na mgogoro wa muda mrefu tangu 2013/2014 kuhusu mipaka, je, Serikali haikuona kwamba kuna haja ya kumaliza ile migogoro kabla ya kuwa na hifadhi ili wananchi waendelee na maisha yao ya kufuga nyuki ambao sasa hivi hawaruhusiwi kufuga mifugo na kulima?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, lini Mheshimiwa Waziri atakuja ajionee mwenyewe kwa sababu mpaka sasa hivi wameshakuja Naibu Mawaziri wawili, alishakuja Mheshimiwa Ramo wakati ule, Mheshimiwa Naibu Waziri Angelina Mabula alikuja na pia alikuja Mheshimiwa Kiwangalla aliyekuwa Waziri lakini bahati mbaya mvua ilinyesha hakuweza kufika maeneo yale. Je, ni lini Serikali inakuja ione jinsi ambavyo wananchi wanataka maeneo waendelee kuendesha maisha yao kwa kilimo, kufuga nyuki na mifugo pia?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusiana na suala la mgogoro, Serikali inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi siku zote imekuwa ikishirikiana na wananchi wake katika kutatua changamoto mbalimbali. Migogoro ya ardhi imeshapatiwa suluhisho kupitia Tume ya Mheshimiwa Rais ya Mawaziri Nane iliyoongozwa na Mheshimiwa Lukuvi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Margaret Sitta kwamba suala hilo nalo limeshapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kuhusiana na lini tutakwenda? Nimhakikishie Mheshimiwa Margaret Sitta mara baada ya Bunge hili nitaambatana naye kwenda jimboni Urambo kuhakikisha tunatatua suala hili. Ahsante sana. (Makofi)