Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 2 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 19 2021-02-03

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MARGARET S. SITTA Aliuliza: -

Serikali imeanzisha Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla Wilayani Urambo: -

(a) Je, ni lini Serikali itatoa elimu elekezi kwa wananchi wa maeneo hayo juu ya matumizi ya eneo husika baada ya mabadiliko yaliyotokea?

(b) Kutokana na ongezeko la watu, je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wananchi maeneo kwa ajili ya ufugaji nyuki, mifugo na kilimo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla ina ukubwa wa kilomita za mraba 3,865. Hifadhi hii ilianzishwa kwa Azimio la Bunge la tarehe 10 Septemba, 2019 na Tangazo la Serikali Na. 936 la tarehe 29 Novemba, 2019. Hifadhi ipo katika Wilaya ya Urambo na Kaliua Mkoani Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, madhumuni ya kuanzishwa kwa hifadhi hii ni kuimarisha uhifadhi ili kuunganisha mfumo wa ikolojia wa Malagarasi - Muyowosi ambao ni ardhi oevu yenye umuhimu wa kitaifa na kimataifa pamoja na kuongeza pato la Taifa kutokana na ongezeko la idadi ya watalii, kuwezesha jamii kunufaika na fursa za utalii na kutunza vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na Mpango kutoa Elimu ya Uhifadhi ambao unalenga kujenga uwezo na uelewa kwa wananchi, viongozi na wadau wengine wa uhifadhi ambao wanapakana na Hifadhi za Taifa. Utekelezaji wa mpango huo, ulianzia kwenye Wilaya ya Kaliua, ambapo ulihusisha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya na vijiji 12. Hatua inayofuatia ni kuendelea na programu hiyo kwenye Wilaya ya Urambo, ambapo zoezi litaanzia kwenye Kata ya Nsendo ambako vijiji nane (8) vitahusishwa. Nia kubwa ya uhamasishaji huo ni kujenga uelewa kuhusu sheria, kanuni na taratibu za uendeshaji wa Hifadhi za Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka 2021/2022, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuendelea kutekeleza mpango wa kutoa elimu ya uhifadhi na kuweka mkazo kwenye kuandaa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya husika, pamoja na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi; kuendelea kuhakiki mipaka ya maeneo ya hifadhi kwa kuweka alama za kudumu na mabango elekezi ili mipaka ionekane kwa urahisi; na kuendelea kutoa huduma za ugani kwa ushirikiano na wadau wa uhifadhi katika maeneo mbalimbali ili kutunza mazingira, vyanzo vya maji na misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungu cha 6 (1) cha Sheria ya Hifadhi za Taifa Tanzania, Sura 282 iliyofanyiwa Mapitio mwaka, 2002 kinabainisha kuwa Mheshimiwa Rais akishatangaza eneo la ardhi yoyote kuwa Hifadhi ya Taifa, haki zote za awali zikiwemo hati miliki zilizokuwa juu ya eneo husika zinakoma. Wizara yangu itawasiliana na Mamlaka za Mikoa na Halmashauri ili kupata maeneo nje ya Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla kwa ajili ya shughuli za ufugaji nyuki, mifugo na kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe wito kwa wananchi wote wanaozunguka Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuzuia na kupambana na ujangili na hatimaye kuboresha utalii kwa ajili ya maendeleo endelevu katika jamii husika na nchi kwa ujumla.