Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Silvestry Fransis Koka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Mjini

Primary Question

MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:- Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa Wananchi wa Kibaha Mjini ambao maeneo yao yalitwaliwa kwa ajili ya mradi wa umeme wa Msongo wa KV 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha?

Supplementary Question 1

MHE. SILVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri na wananchi wa Kibaha Mjini wanaunga mkono jitihada za Serikali za maendeleo hususan katika sekta ya umeme.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo kama unavyoona ni takribani miaka sita sasa na leo ni mara ya nne nauliza swali hili hapa Bungeni. Naomba sasa Mheshimiwa Waziri atoe kauli thabiti kwamba malipo haya kwa wananchi wa Mnalugali, Boko, Sofu, Zegereni watalipwa lini fidia hii ili sasa na wenyewe waweze kushiriki na kufurahia miradi hii mikubwa ya umeme?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, miradi ya umeme katika Mji wa Kibaha na hususan peri-urban na densification imekuwa ikisuasua na haijakamilika. Miradi hii imepita pembezoni mwa wananchi wengi na wanalalamika kwamba hawakuweza kufikiwa na miradi hii. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha sasa miradi hii inakamilika na wananchi wanapata umeme ili kufaidi maendeleo na matunda ya nchi yao?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi la Mheshimiwa Koka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli usanifu wa mradi huo ulianza miaka mingi toka miaka mwaka 2015 na 2016 lakini baadaye tulipoanza kutekeleza mradi mkubwa wa Julius Nyerere mwaka 2018, tulifanya usanifu upya ili kuhakikisha kwamba mradi huu unakuwa ni mpana na endelevu. Mradi huu ambao unahusisha fidia ya wananchi wa Kibaha utahusisha pia fidia ya wananchi wa kutoka Kinyerezi, Kiluvya, Chalinze, Kibaha mpaka kufika Dodoma na unaelekea mpaka Singida.

Mheshimiwa Spika, taratibu kama ambavyo ameeleza Mheshimiwa Naibu Waziri, tumeanza kufanya matayarisho ya malipo na sasa tumetenga shilingi bilioni 21.56 kwa ajili ya kuwalipa wananchi wote. Wananchi wa Kibaha peke yake ambao wanafika 432 wenye jumla ya shilingi milioni 932 malipo yao yameshaanza kutayarishwa. Malipo hayo yanakwenda sambamba na ujenzi wa njia kuu ya kusafirisha umeme kutoka mradi mkuu wa Julius Nyerere utakaofua megawatt 2,115 kutoka Rufiji-Chalinze, Chalinze- Dar es Salaam (kilometa 115) na pia Chalinze-Dodoma, ambapo tumetenga jumla ya shilingi milioni 32.82. Kwa kuwa ujenzi wa mradi wa huu utaanza kabla ya mwezi Juni, ni matumaini yetu na kwa maandalizi mazuri ya watu wa Wizara ya Fedha tutaanza kuwalipa wananchi kabla ya mwezi Juni mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuhusiana na suala la peri- urban na densification, tumeanza programu ya kupeleka umeme kwenye maeneo yote ya ujazilizi. Maeneo ya kutoka Dar es Salaam mpaka hapa Dodoma takriban vitongoji 12,822, utekelezaji umeanza katika maeneo Dar es Salaam hadi Kibaha kwa vitongoji 272 ambapo vitongoji vya Mheshimiwa Koka vimo. Pia tunapeleka umeme kwenye peri- urban anayoizungumza Mheshimiwa Koka kwa maeneo yanayofanana na vijiji ya Kibaha ambayo siyo vijiji kwa kwa gharama ya shilingi 27,000 na utekelezaji umebaki mitaa 12 kati ya mitaa 128. Mradi huu unakamilika mwezi Mei, mwaka huu.

Napenda kumwambia Mheshimiwa Koka awape taarifa wananchi wa Kibaha kwamba peri-urban na densification katika eneo lao inakamilika mwezi Mei, mwaka huu. Ahsante sana. (Makofi)