Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 8 2021-02-02

Name

Silvestry Fransis Koka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Mjini

Primary Question

MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa Wananchi wa Kibaha Mjini ambao maeneo yao yalitwaliwa kwa ajili ya mradi wa umeme wa Msongo wa KV 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha?

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa makofi hayo yanaashiria nyota njema.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa, basi nichukue nafasi fupi kuwashukuru wanachama wa Chama cha Mapinduzi lakini nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi, niwashukuru wana Jimbo la Bukoba Mjini na nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kunipa nafasi hii ya kutekeleza kipande hiki cha majukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvetry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kazi ya uthamini wa mali za wananchi katika mradi wa ujenzi wa njia za kusafirisha umeme kilovoti 400 kutoka Kinyerezi kupitia Kisarawe, Kibaha hadi Chalinze ilifanyika kati ya mwaka 2015 na 2016 ili kuwezesha pamoja na mambo mengine wananchi wanaopitiwa na mradi kulipwa fidia na kupisha ujenzi wa mradi huo. Taratibu zote za uandaaji wa taarifa na majedwali ya fidia zilikamilika mwezi Machi 2020. Fidia kwa ajili ya maeneo kati ya Kiluvya (Kisarawe) hadi Chalinze ni takriban shilingi bilioni 21.569.

Mheshimiwa Spika, aidha, malipo haya yanahusisha Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Chalinze. Kwa sasa taratibu za kuhamisha fedha za fidia kutoka Wizara ya Fedha na Mipango kwenda TANESCO ili kuwalipa fidia wananchi hao zinaendelea. Fidia ya wananchi hao italipwa mara tu baada ya taratibu hizo kukamilika.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Wilaya za Ilala, Ubungo, Kisarawe, Kibaha na maeneo ya Chalinze waliopisha mradi huo kuwa na subira wakati Serikali inakamilisha taratibu za malipo ya fidia kwa wananchi hao.