Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Primary Question

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:- Matatizo ya maji katika Jimbo la Rufiji ni ya muda mrefu kwenye maeneo kadhaa hususan Kata ya Ngarambe maji hupatikana kwa umbali zaidi ya kilometa 7 - 10 na kwa kuwa Serikali sasa inaleta sera ya Maji ndani ya mita 400:- Je, ni lini Serikali itatua kero ya maji katika Kata ya Ngarambe, Mbwala, Chumbi, Muholo, Kipugila na maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Ikwiriri hata kwa kuchimba visima?

Supplementary Question 1

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la maji kwenye Wilaya ya Rufiji ni kubwa sana hali iliyopelekea nguvu kazi kubwa ya vijana na akina mama kupotea wakijaribu kutembea umbali mrefu, pia wakidiriki kuchota maji kwenye maeneo ya Mto Rufiji na kupelekea wananchi wengi kuchukuliwa na Mamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mpango gani wa kuja kufanya tathmini ikizingatiwa kwamba Rufiji ni kanda maalum, pia Rufiji tunatekeleza mradi wa uzalishaji wa umeme wa Stiegler’s Gorge. Je, ni lini Serikali itakuja kufanya tathmini halisi kabisa ya tatizo la maji Wilaya yetu ya Rufiji? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo la maji kwenye Kata ya Mbwala ambayo Mheshimiwa Waziri amejibia ni kubwa sana tofauti kabisa na majibu ambayo wenzetu wa Halmashauri walimwandalia. Eneo kubwa la Kata ya Mbwala wananchi wanalazamika kusafiri umbali wa kilometa saba mpaka 10 kufuata maji katika maeneo ya Kikobo na maeneo mengine.

Je, ni lini Serikali itadhamiria kabisa kuchimba visima virefu karibu na kwa wananchi hali ambayo hivi sasa imepelekea vijiji vingi wananchi kuhama kutafuta maji kwa sababu wanadiriki kusafiri umbali mpaka wa kiklometa 7 - 10?

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Nataka niwahakikishie Wandengereko wote, wamechagua jembe wembe na anafanya kazi kubwa sana katika Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa anataka kujua jitihada za Serikali. Tunatambua kwamba maji ni uhai na ni moja ya changamoto kubwa, lakini sisi kama Wizara ya Maji tumefanya jitihada kubwa ya uchimbaji visima 13 pale yenye thamani zaidi ya shilingi milioni 400, tumeshachimba visima 10. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya ukamilikishaji ule wa visima tutafanya usanifu katika kuhakikisha tunatekeleza miradi mikubwa ili wananchi wako waweze kupata huduma hii ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka nikuhakikishie kutokana na Kata hiyo ya Mbwala, mimi kama Naibu Waziri nitapata nafasi ya kuja katika Jimbo lako na nitafika katika Kata ya Mbwala ili tuweze kushauriana na kuangalia namna gani tunaweza tukatatua tatizo la maji katika kata yako. Ahsante sana.