Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 51 Water and Irrigation Wizara ya Maji 437 2019-06-24

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Primary Question

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:-

Matatizo ya maji katika Jimbo la Rufiji ni ya muda mrefu kwenye maeneo kadhaa hususan Kata ya Ngarambe maji hupatikana kwa umbali zaidi ya kilometa 7 - 10 na kwa kuwa Serikali sasa inaleta sera ya Maji ndani ya mita 400:-

Je, ni lini Serikali itatua kero ya maji katika Kata ya Ngarambe, Mbwala, Chumbi, Muholo, Kipugila na maeneo mbalimbali ya Tarafa ya Ikwiriri hata kwa kuchimba visima?

Name

Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Omary Mchengerwa, Mbunge wa Rufiji, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya huduma ya maji katika Halmashauri ya Rufiji na kwa sasa tayari baadhi ya kata hizo zimeanza kupewa kipaumbele kwa kujengewa miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Mbwala kuna mradi wa kisima kirefu ambao unatumia teknolojia ya dizeli. Mradi huo kwa sasa una changamoto ya uendeshaji kwani wananchi wanatumia gharama kubwa kwa kununua mafuta ya uendeshaji wa mitambo ya mradi huo. Halmashauri inaendelea na taratibu za kutumia teknolojia ya umeme wa REA ambao tayari umeshafika katika kata hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Chumbi vimechimbwa visima viwili ambapo kwa sasa vipo katika hatua ya usanifu wa miradi. Kata ya Muholo imewekwa katika utekelezaji wa miradi ya awamu ya pili ambapo kwa sasa usanifu katika visima viwili umekamilika. Wizara imeshatoa kibali kwa ujenzi wa miundombinu kwani miundombinu ya awali ilichakaa na haifai tena kwa mradi. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya Rufiji imetengewa jumla ya shilingi milioni 871.98 kwa ajili ya kuendelea kukamilisha miradi ya zamani ya kujenga miradi mipya.