Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Haji Khatib Kai

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Micheweni

Primary Question

MHE. HAJI KHATIB KAI aliuliza:- Je, ni sifa gani anastahili kuwa nazo Askari Polisi ili aweze kuteuliwa kuwa OCD?

Supplementary Question 1

MHE. HAJI KHATIB KAI: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninayo masuala mawili ya nyongeza. Mkoa wa Kaskazini Pemba una Wilaya mbili za Kipolisi kwa maana ya Wilaya ya Wete na Wilaya ya Micheweni. Ma-OCD hawa walikaimu au wamekaimu zaidi ya miaka mitatu katika nafasi za OCD mwaka 2016 hadi mwaka 2019 na kwa OCD ya Wilaya ya Wete alikaimu nafasi hiyo hadi pale muda wake wa kustaafu ulipomfikia bila kupata maslahi yoyote ya cheo cha OCD. Mheshimiwa Naibu Waziri je, ni utaratibu gani wa Serikali kupitia Wizara yako inaweza ikafidia ma-OCD kama hawao kaimu bila kupata maslahi ya kazi hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa kukaimu nafasi ya OCD kuna changamoto za kiutendaji na si tu changamoto za kiutendaji hata changamotoza kimazingira. Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa Serikali imekuwa ikitoa kiasi kidogo sana cha mafuta kwa mwezi shilingi 1,000,000 jambo ambalo linamfanya OCD anayekaimu kutumia fedha zake za mfukoni kama Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani na unajua umuhimu wa mafuta kwa Polisi, umesimamiaje Serikali kuhakikisha kwamba inaongeza mafuta ili kuondoa tatizo la mafuta kwa Jeshi la Polisi? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimefarijika kuona Mheshimiwa Kai leo amekuwa mtetezi wa Askari wetu na hii inadhihirisha kwamba kumbe Askari wetu wanafanya kazi vizuri sana kule Pemba, wanashirikiana vizuri sana na Mheshimiwa Kai pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine ambao kwa Pemba tunajua asilimia kubwa Wabunge wanatoka Chama gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo nataka nimjibu kama ifuatavyo. Kwanza hakuna fidia katika kukaimu niseme tu labda nishee pamoja na yeye masikitiko yake kuhusu kukaimu kwa muda mrefu bila kupandishwa cheo. Maana kama amekaimu miaka mitatu maana anaiweza hiyo nafasi lakini nimthibitishie kwamba ili mtu aweze kupanda cheo kuna taratibu ambazo nimezieleza katika jibu la msingi. Na moja katika mambo ambayo yanapelekea vilevile kupandishwa cheo kwa Askari ni kutokana na kuwepo kwa hizo nafasi, sasa inawezekana kwa bahati mbaya katika kipindi hiki ambacho wanakaimu hakukuwepo na fursa za kuweza kupandishwa cheo kwa Askari wahusika. Na kama unavyojua kwamba mahitaji ya Askari ambao wanahitaji kupandishwa cheo ni wengi na wengi vilevile wana sifa, kwa hiyo nafasi ni chache lakini wenye sifa ni wengi na ndio maana tunapandisha kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na bajeti ya mafuta nimuhakikishie kwamba tutajitahidi kadri ya miaka inavyokwenda kulingana na hali ya ukuaji wa uchumi wetu kuongeza bajeti katika Jeshi la Polisi ikiwemo bajeti ya mafuta. Tunatambua kwamba bajeti ya mafuta katika maeneo mengi bado haikidhi lakini tutaendelea kuizidisha katika maeneo yote ikiwemo katika Wilaya ya Micheweni na Wilaya ya Wete ili hatimaye tuweze kuhakikisha kwamba Askari wetu wanafanya kazi zao vizuri na kwa ufanisi.