Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Prof. Jumanne Abdallah Maghembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Primary Question

MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE aliuliza:- Serikali inafanya juhudi katika kuendeleza elimu hapa nchini kwa kutoa elimu bure na hata kujenga Shule nyingi zikiwemo za kata. Je, lini sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kukamilisha Maabara za Sayansi katika Shule zote za kata nchini?

Supplementary Question 1

MHE. PROF. JUMANNE A. MAGHEMBE: Mheshimiwa Spika, nimejibiwa, kwa kuwa nchi yetu itahitaji wanasayansi huko mbele tuendako, na hivi sasa tunavyojenga uchumi wa viwanda. Je, Serikali haioni kwamba hali tuliyonayo katika shule zetu za sekondari ambapo shule za Serikali zina walimu wazuri sana lakini hazina maabara na shule zile za binafsi zina maabara, walimu siyo wazuri kama wale wa Serikali, lakini watoto wale ndiyo wanafaulu mitihani. Serikali ina mpango gani hasa kuhusu kuwaandaa wanasayansi watakaoiendeleza nchi yetu huko mbele? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, nimeona fedha hapa vimetengwa, kwa ajili ya maabara, si maabara peke yake kama ulivyoona swali lenyewe. Nilikuwa nataka nimuulize Waziri, kati ya fedha hizi ni shilingi ngapi zitapelekwa Mwanga kwa ajili ya kusaidia wananchi kujenga maabara ya Msalagambo yale yaliyojengwa sasa?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Profesa ameuliza kwa uchungu na yeye pia ni mwanasayansi ni Profesa katika eneo hilo na tunatambua changamoto iliyopo ya masomo ya sayansi na hasa maabara, lakini niseme, fedha ambazo nimetaja hapa shilingi bilioni 58.2 ni mwaka wa fedha huu 2019/2020, lakini mwaka wa fedha uliopita tumepeleka fedha kwenye shule za sekondari 1964, lakini hapa tulipo tunafanya mchakato wa kupeleka tena fedha za vifaa vya maabara katika shule zetu zaidi ya 2000.

Mheshimiwa Spika, lakini ujue kwamba sisi sekondari za Serikali ni 3632, kwa hiyo tunaamini baada ya mpango huu kukamilika ndani ya mwaka huu mpaka 2020 karibu kila maabara itakuwa na vifaa vya kutosha katika eneo hilo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Profesa nimtoe wasiwasi kwa jambo hili na kwamba tumejipanga namna ya kufanya vuzuri, lakini tumeshatoa maelekezo, maeneo ambayo kuna upungufu wa maabara kuna namna njia mbadala zimefanyika ndiyo maana leo ukiangalia hata pale viwanja vya Jamuhuri kuna maonesho yanafanyika na walimu wetu wamefundishwa kufanya njia mbadala ili tuweze kufundisha watoto wetu kwa vitendo na ufaulu utakuwa unaongezeka kutoka mwaka hadi mwaka.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili la kuuliza, kama ulivyosema, kwamba sina data hapa lakini nadhani baada ya kipindi cha maswali na majibu ninaweza nikampa kumbukumbu, data kamili kwamba yeye katika eneo lake la Mwanga atapata shilingi ngapi katika shule aliyoitaja, ahsante.