Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR (K.n.y MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOSS NYIMBO) aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka uzio kwenye vituo vikubwa vya Polisi vilivyopo Zanzibar?

Supplementary Question 1

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza:-
Kwa kuwa, Naibu Waziri amekiri kwamba wameshaanza kujenga uzio katika kituo cha Ziwani pale Zanzibar, tunashukuru sana Serikali. Naomba kumuuliza sasa, Zanzibar ina vituo vingi sana ikiwemo na vituo vya Pemba, je, ni lini Seriali itajenga uzio katika vituo vya kule Pemba?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amejibu kwamba itajenga uzio katika maeneo mbalimbali ya Tanzania, ninavyoelewa kwamba bila ya bajeti uzio hizo hazitoweza kujengwa na hatujaona katika bajeti yake kukiwemo ni makisio hayo. Je, Serikali itakubaliana na mimi kwamba katika mwaka ujao wa 2017/18 iweze kuweka bajeti ya kuwajengea uzio katika vituo mbalimbali na makambi ya Polisi. Ahsante.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza kwamba ni lini vituo vitajengewa uzio. Kama ambavyo nimekuwa nikizungumza kila siku kwamba ujenzi wa uzio, ukarabati wa vituo na kadhalika inategemeana na uwezo wa kifedha. Hata hivyo, kwa kuwa malengo ya kujenga vituo ambavyo kwa mujibu wa PGO namba 287 inaonesha kwamba maeneo ambayo vituo vinavyohitaji kujengewa uzio ni vituo class (a) na (b), lakini kwa mujibu wa PGO namba 314 vilevile inaonesha dhamira ya ujenzi wa uzio ni kuhakikisha usalama unaimaridhwa katika maeneo husika.
Hata hivyo kwa kukidhi ile PGO 314 ni kwamba unaimarisha ulinzi katika maeneo hayo katika kipindi hiki ambako bado bajeti haijaweza kukidhi kujenga vituo vyote. Kwa hiyo, kimsingi ni kwamba tunaweza kutekeleza hili jambo la kuimarisha usalama katika vituo vyetu kwa kuimarisha ulinzi. Kwa kuanzia wakati huo huo tunatafuta fedha za kuweza kujenga uzio.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni kwamba anajaribu kupendekeza bajeti ya mwaka ujao wa fedha tuweze kuwa na bajeti ya kutosha kwa ajili ya kujenga uzio. Mimi naamini kabisa chini ya utaratibu ambao Serikali hii ya Awamu ya Tano tunakwenda nao ya kuhakikisha kwamba tunaongeza kukusanya mapato katika nchi hii, basi imani yangu ni kwamba kadri ya miaka inavyokwenda mbele tunaweza kupata bajeti ya kutosha na Wizara ya Mambo ya Ndani kuweza kukabiliana na changamoto mbalimbali ikiwemo ujenzi wa uzio katika vituo vyetu vya Polisi.