Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mary Pius Chatanda

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Korogwe Mjini

Primary Question

MHE. MARY P. CHATANDA aliuliza:- Umeme umekuwa ukikatika mara kwa mara Korogwe na kufanya uharibifu wa mali za Wananchi:- Je, ni lini tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi.

Supplementary Question 1

MHE. MARY P. CHATANDA Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafas niulize swali la nyongeza. Nichukue nafasi hii kuishukuru Wizara ya Nishati kupitia Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wa TANESCO Mkoa na Wilaya ya Korogwe kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya sasa ya kuhakikisha kwamba vijiji vinapata umeme wa REA katika maeneo yale ambayo yalikuwa yamekosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la nyongeza ni kwamba; kwa kuwa adha hii imekuwa ni ya muda mrefu na majibu aliyoyatoa Naibu Waziri ni mazuri, yanaridhisha:

Je, ni lini sasa ukarabati huu utakamilika? Maana unaweza ukasema unaendelea kukarabati, halafu inaweza ikawa mwaka mzima unafanyika ukarabati. Ni lini sasa watakamilisha ukarabati huu ili kusudi wananchi waondokane na adha hii ambayo wanaipata sasa? (Makofi)

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimepokea kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri shukrani zake, lakini kipekee nampongeza Mheshimiwa Chatanda kwa kazi nzuri anayofanya kwenye Jimbo lake, lakini kwa ushirikiano wake pamoja na ofisi yetu ya TANESCO ya Mkoa na Wilaya ya Korogwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu letu la msingi ni kwamba kwanza ukarabati huu ni mkubwa, unahusisha nguzo zaidi ya takriban 920 na unagharimu shilingi bilioni 1,400. Mpaka sasa zaidi ya nguzo 500 zimesharekebishwa, zimeondolewa zile mbovu na zimewekwa hizo mpya. Nataka nimwambie, matarajio yalikuwa tukamilishe mwezi huu Januari mwishoni na huu wa Pili unaoendelea, lakini kwa kuwa mvua zinaendelea, tumeongea na TANESCO tukiwaelekeza kwamba pamoja na changamoto ya mvua, lakini waendelee kufanya haraka kukamilisha nguzo takribani 400 zilizobaki ili wananchi wa Korogwe vijijini na mjini wapate umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Mama Chatanda amekuwa akiambatana na TANESCO Wilaya katika maeneo hayo na mwenyewe amejionea. Kwa hiyo, niendelee tu kuwapa pole wananchi wa Korogwe, lakini dhamira ya Serikali kupitia Shirika la
TANESCO ni kuhakikisha umeme unapatikana wa uhakika na muda wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. MARY P. CHATANDA aliuliza:- Umeme umekuwa ukikatika mara kwa mara Korogwe na kufanya uharibifu wa mali za Wananchi:- Je, ni lini tatizo hilo litapatiwa ufumbuzi.

Supplementary Question 2

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa niulize swali moja la nyongeza. Matatizo ya Korogwe Mjini yanafanana sana na matatizo ya Wilaya ya Rungwe hususan Busokelo kwa kukatika katika umeme. Kwa siku umeme unaweza kukatika zaidi ya mara 10 na tatizo kubwa lililokuwepo ni kwamba, nguzo za umeme chini yake kuna miti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Wizara pamoja na Waziri kwa maana ya kuleta timu maalum kwenda ku-clear ama kukata hiyo miti, lakini bado tatizo kubwa limeendelea kuwepo. Ni mikakati gani Serikali iko nayo kuhakikisha kwamba wananchi wa Jimbo la Busokelo wanapata umeme masaa 24 kwa siku kuliko hivi ilivyo kwa sasa? (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri katika swali la msingi, lakini hata la nyongeza kwa Mheshimiwa Chatanda; na niendelee kumpongeza Mheshimiwa Mwakibete kwa swali linalofafana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Shirika letu la umeme nchini na kwa niaba ya Serikali, napenda tu nisema mambo mawili kwamba ukarabati unaoendelea. Jambo la kwanza tumetenga kila Mkoa wa ki-TANESCO kwa nchi nzima takriban shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kufanya ukarabati mkubwa.

Kwa hiyo, wananchi katika maeneo yote ya mikoa yetu ambayo kuna kero ya kukatika kwa umeme, kwanza haukatiki kwa sababu ya hali ya umeme, isipokuwa tunakata kufanya matengenezo. Kwa hiyo, naomba nitoe taarifa hiyo kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tumetoa muda mahususi wa miezi sita kukamilisha ukarabati wote kwa nchi nzima. Kwa hiyo, ni matumaini yetu Mheshimiwa Mwakibete katika eneo lake ambalo lilikuwa na kero kubwa sana ndani ya miezi sita ukarabati utakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, tumeleta transforma kubwa, tunabadilisha transformer kutoka ndogo kwenda kubwa, kwa sababu shughuli za uchumi za wananchi zinaongezeka. Kwa hiyo, tunaomba radhi kwa wananchi wote ambako ukarabati unaendelea. Tunaomba mtuvumilie tukamilishe kazi hiyo. Ahsante sana.