Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:- Serikali hupeleka katika Halmashauri zilizopo katika Hifadhi ya Wanyamapori asilimia 25 ya fedha zitokanazo na mapato ya uwindaji wa kitalii na upigaji picha pasipo Halmashauri husika kujua msingi wa tozo hizo. • Je, ni lini Serikali itaanza kupeleka takwimu ya mapato yanayopatikana ili Halmashauri ziweze kujua stahiki zake? • Je, ni kiasi gani cha mapato kimepatikana kutokana na Maswa Game Reserve na Hifadhi ya Makao na kiasi gani kilipelekwa katika Wilaya ya Meatu kila mwaka kuanzia mwaka 2015 hadi 2017?

Supplementary Question 1

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali kwamba asilimia 40 ifanye kazi ya uhifadhi. Vile vile kwa mujibu wa waraka asilimia 60 inatakiwa iende katika vijiji vinavyopakana na hifadhi ambavyo ni Mwambegwa, Mwanyaina, Mwagwila, Semu, Nyanza, Matale na vingine vingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2016/2017 vijiji vile havikupelekewa hela na asilimia 40 haikufanya kazi ya uhifadhi na hivyo kuipelekea Idara ya Wanyamapori kushindwa kununua silaha kwa ajili ya kukabiliana na wanyamapori. Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya zile fedha zikapelekwa moja kwa moja katika vijiji na asilimia 40 ikapelekwa katika Pori la Akiba kuliko kupelekwa Akaunti ya Amana? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, asilimia 44 ya kilometa za mraba ya Wilaya ya Meatu ni hifadhi. Halmashauri imepata ugumu katika kukabiliana na ujangili, uhifadhi wa maliasili na uvamizi wa wanyamapori kwa sababu ina changamoto ya vitendea kazi. Je, Serikali iko tayari kuipatia gari Wilaya ya Meatu? (Makofi)

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Leah kwa jinsi ambavyo amekuwa akifanya kazi na kufuatilia masuala mbalimbali yanayohusu Jimbo lake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali asilimia 60 zinazobaki kule kwenye Halmashauri kwamba ziende kwenye vijiji kama alivyosema, ni wajibu kila Halmashauri zinazopata mgao huu ile asilimia 60 inatakiwa iende katika vile vijiji vinavyozunguka hifadhi, kwa sababu zinatakiwa zitumike katika kuleta maendeleo ya vijiji vile vinavyohusika. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuziomba Halmashauri zote nchini kutekeleza hilo agizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kuhusu maombi ya gari, naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba ni kweli kabisa kumekuwa na changamoto katika lile eneo na Wizara yangu inazo taarifa za kutosha. Tutalifanyia kazi maadam amelileta, tutaona pale hali itakaporuhusu kifedha tutawapelekea gari lile ambalo litawasaidia katika shughuli hizo. (Makofi)