Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 30 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 257 2018-05-16

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-
Serikali hupeleka katika Halmashauri zilizopo katika Hifadhi ya Wanyamapori asilimia 25 ya fedha zitokanazo na mapato ya uwindaji wa kitalii na upigaji picha pasipo Halmashauri husika kujua msingi wa tozo hizo.
• Je, ni lini Serikali itaanza kupeleka takwimu ya mapato yanayopatikana ili Halmashauri ziweze kujua stahiki zake?
• Je, ni kiasi gani cha mapato kimepatikana kutokana na Maswa Game Reserve na Hifadhi ya Makao na kiasi gani kilipelekwa katika Wilaya ya Meatu kila mwaka kuanzia mwaka 2015 hadi 2017?

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imekuwa ikitoa mgao wa asilimia 25 ya mapato yatokanayo na ada za wanyamapori wanaowindwa kwenye vitalu vilivyopo kwenye maeneo ya Wilaya husika. Katika mwaka wa fedha 2015/2016 na 2016/2017 Wilaya ya Meatu ilipata mgao wa shilingi 40,017,158 na shilingi 41,696,616.43 sawia ikiwa ni asilimia 25 ya mapato yatokanayo na wanyamapori waliowindwa katika vitalu vya Mbono na Kimali katika Pori la Akiba la Maswa na Makao WMA.
Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za mapato yanayotokana na wanyamapori waliowindwa na upigaji picha katika vitalu vya uwindaji na utalii wa picha nchini huandaliwa na kutolewa taarifa mbalimbali. Aidha, Wizara ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha mfumo wa kielektroniki ujulikanao kama MNRT Portal ambapo taarifa zinazohusu Wizara ikiwa ni pamoja na mapato ya uwindaji wa kitalii zitapatikana humo. Mfumo huo unatarajiwa kuzinduliwa rasmi tarehe 1 Julai, 2018. Aidha, nakala ngumu zitatumwa kwenda Wilaya husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe wito kwa Halmashauri nchini zinazopata mgao huu kutumia asilimia 40 ya fedha hizo kwa ajili ya shughuli za uhifadhi ikiwa ni pamoja na ulinzi wa maisha ya wananchi na mali zao dhidi ya wanyamapori wakali kama ilivyokubalika.