Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Primary Question

MHE. DKT. MARY M. NAGU aliuliza:- Afya ni uhai na ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata afya bora katika Wilaya ya Hanang:- (a) Je, ni lini Serikali itaziba upungufu wa watumishi wa afya katika Wilaya ya Hanang ambao wamefikia watumishi 202 hadi sasa? (b) Je, ni lini Serikali itafungua duka la MSD na kuboresha vifaa tiba kwenye vituo vya afya katika Wilaya ya Hanang? (c) Je, ni lini Serikali itajenga wodi zaidi za akina mama na watoto katika Hospitali ya Wilaya ya Tumaini iliyopo Hanang ili kupunguza msongamano katika Wodi hizi?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jibu zuri alilotoa. Pamoja na jibu hilo, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Kwanza, Hanang ni Wilaya ya pili kuwa na CHF iliyoboreshwa na CHF hii iliyoboreshwa haitaweza kunufaisha wananchi kama hakutakuwa na dawa za uhakika. Je, Serikali haioni ni vizuri pamoja na CHF iliyoboreshwa kuwe na duka la MSD?
Pili, Wilaya ya Hanang ina upungufu wa Wodi za akina mama na watoto na nimeshukuru sana kuona kwamba wodi ambayo italaza wanawake 16 inajengwa, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba ni wanawake 200. Je, kuwa na wodi itakayolaza wanawake 16 itatosheleza mahitaji hayo?
Pamoja na hivyo, naomba Serikali ione umuhimu wa Wilaya ya Hanang ambayo imezungukwa na Wilaya nyingi kuwa na wodi za kutosheleza akina mama kulazwa.

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, kwanza siyo CHF peke yake iliyoboreshwa kwa Halmashauri ya Hanang, lakini kubwa zaidi napenda kumpongeza Mbunge huyu kwa sababu katika michakato yao ya kuhakikisha kwamba huduma ya afya inaimarika huko Hanang kwamba japo wana vituo vya afya vinne, lakini sasa hivi wanaendelea na ujenzi wa vituo vya afya sita. Kwa hiyo, naomba nimpongeze sana katika hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kweli tumesema kwamba sasa hivi dawa zinapatikana kule Kilimanjaro na lengo ni kwamba kuhakikisha maduka ya dawa haya yanapatikana kila eneo; nilisema pale awali, tatizo kubwa ni changamoto ya bajeti, lakini nadhani kwa kadri tunavyokwenda, tutaangalia jinsi gani tutafanya kila maeneo maduka ya madawa haya yaweze kupatikana ilimradi kuwapelekea wananchi huduma kwa karibu zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la wodi ya wazazi, ni kweli kwamba ile haitoshelezi, lakini watu wanasema angalau tuna sehemu tumeanza. Sasa hivi kuna wodi ya wazazi ndani ya kipindi hiki cha mwaka 2016 na wodi ile itakamilika ambayo itakuwa ina uwezo wa kuchukua akina mama 16.
Lengo la Serikali ni kwamba tunatafuta fursa zote zinazowezekana ili mradi eneo lile ambalo population yake ni kubwa zaidi, kuhakikisha kwamba tunapata fursa mbalimbali za kuongeza nguvu angalau kuhakikisha wodi hizi zinaongezeka. Siyo Hanang peke yake, isipokuwa Tanzania nzima changamoto za wodi zimekuwa ni kubwa, lakini ni jukumu la Serikali kuangalia tunafanya vipi sasa ili mradi huduma ya afya iweze kuimarika na hususan tukiangalia Bajeti ya mwaka huu ya Wizara ya Afya ambayo itakuja, Waziri atakuja hapa kuelezea jinsi gani bajeti imejielekeza sasa katika miradi ya maendeleo kwa kiwango kikubwa sana ukilinganisha na pale awali.