Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 10 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 72 2016-05-02

Name

Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Primary Question

MHE. DKT. MARY M. NAGU aliuliza:-
Afya ni uhai na ili kuhakikisha kwamba wananchi wanapata afya bora katika Wilaya ya Hanang:-
(a) Je, ni lini Serikali itaziba upungufu wa watumishi wa afya katika Wilaya ya Hanang ambao wamefikia watumishi 202 hadi sasa?
(b) Je, ni lini Serikali itafungua duka la MSD na kuboresha vifaa tiba kwenye vituo vya afya katika Wilaya ya Hanang?
(c) Je, ni lini Serikali itajenga wodi zaidi za akina mama na watoto katika Hospitali ya Wilaya ya Tumaini iliyopo Hanang ili kupunguza msongamano katika Wodi hizi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mary Michael Nagu, Mbunge wa Hanang, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Hanang ina upungufu wa watumishi wa afya 456. Katika mwaka wa fedha 2015/2016 Halmashauri imeidhinishwa kibali cha kuajiri watumishi 64 ambao wataajiriwa muda wowote katika Halmashauri hiyo. Vilevile katika mwaka wa fedha 2016/2017 wameomba watumishi wengine 59 wa kada mbalimbali za afya.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka kipaumbele kwa kufungua maduka ya dawa kwenye Hospitali za Rufaa za Mikoa kutokana na upungufu na ufinyu wa bajeti. Maduka hayo ya Bohari ya Taifa ya Dawa (MSD) yatafunguliwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Mkoa wa Manyara na Halmashauri zake inaendelea kuhudumiwa na Bohari ya Taifa ya Dawa (MSD) iliyoko Mkoa wa Kilimanjaro.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, wodi moja ya wazazi iliyoko katika Hospitali ya Wilaya ya Hanang haikidhi mahitaji kutokana na idadi kubwa ya wazazi wanaofika Hospitalini hapo kujifungua. Kwa mwezi wodi hiyo inapokea takribani wazazi 200 wengine kutoka Wilaya jirani. Serikali kwa kushirikiana na Shirika la EngeredHealth inaendelea na ujenzi wa wodi mpya moja ambao utakamilika kwa mwaka huu wa 2016.
Mheshimiwa Naibu Spika, jengo hilo litakuwa na uwezo wa kulaza akina mama wajawazito 16 kwa wakati mmoja. Vilevile katika mwaka wa fedha 2015/2016, Halmashauri imetenga shilingi milioni 70 kupitia ruzuku ya maendeleo katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya wazazi ambapo fedha hizo bado hazijapokelewa.