Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Cosato David Chumi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafinga Mjini

Primary Question

MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:- Wanariadha wa baadhi ya nchi ambazo kijiografia mazingira yao yanafanana na baadhi ya maeneo katika nchi yetu wamekuwa wakishiriki katika mashindano ya riadha ya majiji makubwa duniani kama vile New York Marathon, Tokyo Marathon na kadhalika na hivyo kuzitangaza nchi zao ipasavyo. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa inafufua mchezo wa riadha ili kutumia kutangaza utalii wa nchi yetu?

Supplementary Question 1

MHE. COSATO DAVID CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Mwakyembe nilimuona ameenda kumtembelea yule nahodha wa Serengeti Boys ambaye aliumia wakati wa mashindano ya Gabon. Hilo ni jambo jema maana linawatia moyo sana vijana wetu.
Mheshimiwa Spika, sasa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, wakati Alphonce Simbu anakwenda kushiriki mashindano kule London Marathon, kati ya magumu aliyokutana nayo ni suala zima la yeye kusaidiwa katika kupata visa. Simbu aliondoka hapa Alhamisi kupitia Afrika Kusini na kwenda kushiriki mashindano siku ya Jumapili, kitu ambacho kilimuathiri sana katika performance yake. Kama angeweza kuondoka mapema maana yake angeweza hata kuwa mshindi kuliko kushika nafasi ya tano. (Makofi)
Swali, je, Serikali iko tayari kuwasaidia wanariadha ambao wame-qualify kwenda kushiriki mashindano makubwa ya Kimataifa katika kuhakikisha kwamba wanapata visa kwa wakati? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama nilivyosema, mchezo wa riadha hasa katika kushiriki mashindano makubwa ya marathon kwa mfano, Tokyo Marathon inavutia watazamaji wa barabarani yaani wakati mbio zinakimbiwa kiasi cha watu milioni 1.7. London Marathon watu 800,000 wanakuwa wanashuhudia barabarani, Boston Marathon watu milioni moja.
Swali, je, Serikali ipo tayari kugharamia maandalizi ya wanariadha wetu ambao wanakuwa wame-qualify kwenda kushiriki mashindano haya makubwa ambayo kwa namna moja au nyingine watasaidia kutangaza Taifa letu katika utalii? (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nianze kwa kupokea pongezi za Mheshimiwa Waziri wangu Dkt. Harrison Mwakyembe kutoka kwa Mheshimiwa Chumi, nitamfikishia salamu hizi. Vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Chumi, kwa kujali kanuni na kujikita katika maswali ambayo yapo ndani ya swali la msingi, ambayo yanahusu riadha, namshukuru sana na ninampongeza. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, Vile vile nimpongeze sana kwa sababu yeye ni mwanariadha wa vitendo, kila siku asubuhi huwa tunakutana naye katika uwanja wa Jamhuri akikimbia. Nina imani kabisa kwamba sasa hivi anaweza akawa anakidhi vigezo vya mashindano ya kimataifa.
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo.
Mheshimiwa Spika, kwanza nikubaliane naye kwamba kweli huyu Alphonce Simbu wakati anakwenda katika mashindano ya London alipata matatizo ya kupata visa. Hata hivyo baadaye alifanikiwa kutokana na Serikali kuingilia kati zoezi hili.
Mheshimwia Spika, sasa niseme tu kwamba, mashindano haya huwa yanasimamiwa na vyombo mbalimbali. Kuna yale mashindano ambayo yanasimamiwa na International Federations lakini yapo mashindano ambayo yanasimamiwa na Olympic Committees. Kwa mfano, yapo mashindano ambayo yanasimamiwa na Shirikisho la Riadha la Taifa, lakini pia mashindano ambayo yanasimamiwa na Tanzania Olympic Committee (TOC). Sasa haya ni yale ya Jumuiya ya Madola na yale ya Olympic. Ukiangalia mwanzoni Simbu hakupata matatizo wakati wanakwenda kwenye mashindano ya Olympic, ni kwa sababu hii TOC ilifanya maandalizi mapema.
Mheshimiwa Spika, sasa haya mashindano yake ya pili ni kwamba alichelewa na kwa maana hiyo, napenda kutoa wito kwa wanariadha wote ambao wanapata sifa au vigezo vya kushiriki mashindano yoyote ya kimataifa au kupata mialiko yoyote ya kushiriki mashindano ya kimataifa, wale mawakala au mameneja wao au mashirikisho au pengine vyama, tunavishauri viwasiliane na Serikali mapema ili kusudi Serikali iweze kufanya mipango na kuwasiliana na maafisa wetu wa Ubalozi na kuondoa usumbufu huu ambao ameusema; kwamba wakati mwingine unasababisha mtu kutokufanya vizuri. Kwa hiyo Serikali tukipata taarifa mapema, tunaweza tukasaidia kwa haraka sana ili kusudi mshindanaji na mchezaji ule aweze kupata visa mapema.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili linauliza kama Serikali ipo tayari kugharamia maandalizi. Maandalizi kimsingi yanafanywa na vyama, vilabu na mashirikisho. Kwa kuzingatia kwamba michezo hii ni mali ya jamii na wanamichezo wenyewe wanatokana na jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nirudie tu kusema kwamba maandalizi yanapofanyika mapema, na hasa ile mipango ya vyama au mashirikisho, inapotufikia Serikalini mapema inakuwa ni rahisi kwetu kujua wale wamekwama wapi, wanamikakati gani na hivyo tunaweza tukasaidia katika maandalizi.
Mheshimiwa Spika, kwa mfano tu niseme kuna wanariadha ambao wanatarajia, wanavigezo vya kwenda kufanya mashindano ya Common Walk Games Australia mwezi wa nne ambapo wako sita. Tumeshaanza kufanya mazungumzo na Serikali ya Ethiopia ili kusudi waweze kuweka kambi ya miezi nane kule Ethiopia na kupata utaalam na kuweza kufanya vizuri katika mashindano hayo. Hata hivyo tuko katika utaratibu wa kutafuta vyanzo endelevu vya mapato ili kuweza kuwasaidia wanamichezo wote siku za baadaye. Ahsante. (Makofi)