Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini mradi wa umeme wa REA utaanza kutekelezwa katika Jimbo la Busanda?

Supplementary Question 1

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimwia Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa kwa muda mrefu sana kuna baadhi ya sehemu kwa mfano ndani ya Jimbo la Busanda wana umeme, lakini katika Taasisi za Serikali na za Umma hazijaweza kufikiwa na umeme huo. Nikitoa mfano, Kituo cha Afya Bukoli, Kituo cha Afya Lwamgasa, Shule ya Sekondari ya Bukoli, Shule ya Sekondari Lwamgasa, Shule ya Sekondari Chigunga na kwenye Zahanati ya Chigunga umeme huu haujafika.
Je, Serikali inasemaje sasa kuhusu mpango wa kuhakikisha kwamba Taasisi zote za Umma pamoja na sehemu za kuabudia zinafikiwa na umeme wakati utekelezaji unapoendelea? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tumeona katika vyombo vya habari katika mikoa mbalimbali umeme ukizinduliwa ili Awamu ya Tatu ya REA iweze kuanza kufanya kazi lakini katika Mkoa wa Geita sijaona jambo hili likifanyika. (Makofi)
Je, ni lini sasa Serikali itazindua rasmi umeme wa REA Awamu ya Tatu katika Mkoa wa Geita ili wananchi waweza kuanza kuona utekelezaji wake? (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kumpa pole sana Mheshimiwa Bukwimba kwa wananchi wake wanne walioangukiwa na kifusi kwenye machimbo ya kule Nyamalimbe, pole sana Mheshimiwa Bukwimba kwa niaba ya wananchi wa Geita.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyouliza Mheshimiwa Bukwimba, nianze kwanza kumpongeza anavyouatilia maendeleo ya umeme kwa wananchi wa Jimbo la Busanda. Hata hivyo, mradi kabambe wa REA Awamu ya Tatu, kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi unalenga kupeleka umeme katika vijiji vyote vilivyobaki lakini katika vitongoji vyote vilivyobaki na taasisi za umma. Nisisitize katika hili, Taasisi za Umma ninamaanisha vituo vya afya, shule, misikiti, masoko na kadhalika, haya yote yatafikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Bukwimba, vijiji vyake vya Nyaluyeya ambavyo vituo vya afya havina umeme sasa vitawekewa umeme. Kule Nyamalimbe vituo vya afya pamoja na shule vitawekewa umeme. Shule za Bukoli, shule za Kamena, Kaseme pamoja na vituo vya kwa Mheshimiwa Musukuma, kisiwa chake cha Izumachele tutaenda mpaka huko.
Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa wa Busanda kwamba vitongoji vyote ambavyo vina zahanati tutawekea zahanati umeme pamoja na shule. Umeme mwingine mbadala, kwenye taasisi za umma tutawawekea pia umeme wa solar. Hii ni kwa sababu ikitokea kuna hitilafu ya umeme basi umeme wa solar uweze kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, ni lini sasa tunazindua, nitumie nafasi hii kusema kwamba ni kweli tumezindua mikoa kumi tu nchi nzima, tunaendelea kuzindua mikoa yote 15 iliyobaki ya Tanzania Bara, mkoa mmoja hadi mwingine na mahali pengine ikilazimika tutazindua kila wilaya ili wananchi waweze kujua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumueleza Mheshimiwa Lolesia Bukwimba kuanzia mwezi wa saba tutaanza uzinduzi, kwa hiyo, mwezi wa saba Mheshimiwa Bukwimba tufuatane ili tukazindue umeme wa REA Awamu ya Tatu katika Jimbo lako.

Name

Halima Abdallah Bulembo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini mradi wa umeme wa REA utaanza kutekelezwa katika Jimbo la Busanda?

Supplementary Question 2

MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Kyerwa Mkoani Kagera kuna vijiji ambavyo vimewekwa katika mpango wa Rea Awamu wa Pili, vijiji kama Songambele, Kitwe, Mulongo lakini havikupatiwa umeme. Vijiji hivi hivi pia vimewekwa katika Mpango wa REA Awamu ya Tatu. Je, Serikali itahakikisha katika Mpango huu wa REA Awamu ya Tatu, vijiji hivi havitakosa umeme? (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji vya Kyerwa ambapo vimebakia 27 vitapelekewa umeme vijiji vyote na siyo tu vijiji ambavyo umetaja vya Mulongo pamoja na Songambele lakini viko vijiji na chuo vya ufundi pale Kyerwa na chenyewe tutakipelekewa umeme. Kwa hiyo vijiji vyote 27 vilivyobaki vitapelekewa umeme katika mradi wa REA Awamu ya Tatu.

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA aliuliza:- Je, ni lini mradi wa umeme wa REA utaanza kutekelezwa katika Jimbo la Busanda?

Supplementary Question 3

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Natambua katika Mkoa wa Mbeya tayari REA Awamu ya Tatu imeishazinduliwa, lakini kuna changamoto kubwa sana katika Wilaya ya Rungwe katika vijiji vya Lupoto, Katabe na Ibungu mpaka sasa hawajapata umeme na hatujajua ni lini watapata. Naomba majibu ya Serikali tuweze kujua ni lini Wilaya hizi zitapata umeme wa REA? Ahsante.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa Mheshimiwa Mbunge nakushukuru ulivyouliza, hapa tunapoongea katika kijiji cha Lugota wakandarasi wanaendelea na kazi, kwa hiyo wanaendelea kupata umeme, lakini vijiji vya jirani pia tutavitembelea ambavyo bado lakini vijiji vyote ulivyotaja kwenye eneo lako vitapata umeme wa REA na umeanza mwezi wa tatu na kwako wewe utakamilika mwakani mwezi wa saba.