Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:- Timu yetu ya Taifa imeendelea kufanya vibaya katika michezo ya kimataifa. Je, Serikali imeliona hilo na imechukua hatua gani?

Supplementary Question 1

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri katika swali ambalo nimeshawahi kuliuza leo ni mara ya tatu, naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa nilishawahi kuishauri Serikali kwamba moja ya sababu kubwa ambayo inasababisha timu yetu ya Taifa kutokufanya vizuri ni utitiri wa wachezaji wa kigeni kwenye nchi yetu na tulipoanza kwanza walikuwa wanaruhusiwa wachezaji watatu, baadae wakaongeza wakwa watano, leo ni saba. Sasa tunategemea Taifa Stars itafanya vizuri? Ningeshauri Serikali wapunguze idadi ya wachezaji wa kigeni abaki moja au wawili kwa sababu sisi tuna wachezaji wetu. (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa Bunge lilishawahi kutunga sheria ya kutenga fedha kutoka kwenye michezo ya kubahatisha kwenda kusaidia michezo ni kwa nini basi hizo fedha zimekuwa hazipelekwi ili kusaidia michezo maana sasa hivi ni sawasawa unakwenda benki kuchukua fedha wakati hujaweka pesa, usitegemee kama utapata. Naomba majibu.

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameonesha kwamba sababu mojawapo ya kushindwa kimichezo hasa mchezo wa soka ni utitiri wa wachezaji wa kigeni na kwamba pengine tupunguze idadi.
Mheshimiwa Spika, kwanza nimtaarifu tu Mheshimiwa Venance kwamba ni kweli wapo wachezaji wa nje takribani 40 katika timu zetu, lakini wachezaji wetu kwenda nje wako 14 tu. Kulingana na concern yake aliyoionesha ni kwamba sasa hivi tuko katika mchakato wa kupitia upya Sera ya Michezo ambapo maoni yanatolewa na wadau wengi na tunalichukulia hili kama ni maoni ya wadau akiwa mdau mmojawapo mzuri sana wa michezo. Kwa hiyo, katika kupitia sera hiyo ambayo iko katika hatua nzuri ambapo tunaiandaa sasa iende katika ngazi za juu zaidi, tutayachukua maoni yote kulingana na suala lake ambalo amelionesha ili tuweze kulifanyia kazi vilevile.
Mheshimiwa Spika, pili kuhusu kutenga fedha za michezo ya kubahatisha ni kweli kipindi cha nyuma hili suala lilikuwa halifanyiwi kazi japo linatakiwa kisheria, lakini kwa bahati nzuri napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kuanzia mwezi wa saba fedha hizi zimetoka rasmi na zimekwenda BMT na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia sasa BMT itakuwa ikipata fedha za Bahati Nasibu ya Taifa. Lakini sio hivyo tu, tunalifanyia kazi ili kusudi michezo yote ya kubahatisha itoe kiasi cha fedha kwenda BMT ili kusaidia maendeleo ya michezo.
Mheshimiwa Spika, kabla sijamalizia nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Venance Mwamoto kwa jinsi alivyokuwa mdau wetu mzuri wa ukweli katika sekta ya michezo kwa jinsi alivyoshiriki, ameshirikiana na BMT kutatua mgogoro wa timu ya Lipuli ambayo sasa baada ya mgogoro huo kutatuliwa inaendelea vizuri na anifikishie salamu zangu kwa Serikali ya Mkoa vilevile. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, pia niwapongeze Waheshimiwa Wabunge ambao wameshiriki katika kuendesha ligi katika maeneo yao ikiwa ni pamoja na yeye Mheshimiwa Venance Mwamoto nawapongeza sana, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Naibu Spika wetu, Mheshimiwa Flatei G. Massay, Mheshimiwa Ritta Kabati, Mheshimiwa Silvestry Koka na Waheshimiwa Wabunge wengine na niwaombe tuige mfano huu lakini kuna wengine ambao bado hawajajitokeza kutuambia lakini wanafanya zoezi hili. Nakushukuru sana.(Makofi)

Name

Flatei Gregory Massay

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:- Timu yetu ya Taifa imeendelea kufanya vibaya katika michezo ya kimataifa. Je, Serikali imeliona hilo na imechukua hatua gani?

Supplementary Question 2

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza, Kwa kuwa, Serengeti Boys vijana wale walionesha umahiri mkubwa wa kiwango kile cha soka kinachotakiwa na wakatutangaza sana kule nje na sasa wamerudi. Je, Wizara ina mpango gani sasa kuwaendeleza vijana hawa ili kutokuwa na ile kazi ya zimamoto, wachezaji hawa wakaendelea kufanya vizuri wakati mwingine wa ligi za kimataifa. (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serengeti Boys imefanya vizuri na imetoa mfano mzuri katika timu za Taifa under seventeen, lakini nadhani sote tunakumbuka kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu hapa alipokuwa akifunga Bunge tarehe tano mwezi wa saba alitoa maagizo kwa TFF kwamba wawatunze vijana hawa wasiwaache wakapotea. Kwa hiyo, sisi kama Serikali/Wizara tulichokifanya ni kuwachukua vijana hawa na kuwaunganisha na majeshi. Kwa hiyo, mpaka sasa wanatunzwa katika kituo cha JKT na pale wanafanya mazoezi ya kila siku na baadae tunaweza kuwatumia katika timu za wakubwa za Taifa. Ahsante.

Name

Anna Joram Gidarya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO aliuliza:- Timu yetu ya Taifa imeendelea kufanya vibaya katika michezo ya kimataifa. Je, Serikali imeliona hilo na imechukua hatua gani?

Supplementary Question 3

MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri.
Mheshimiwa Waziri kumekuwa na tatizo la viwanja katika maeneo mengi, kwa mfano Mkoa wetu wa Manyara ni Mkoa unaoongoza Tanzania nzima kwa kuiletea nchi hii medali hasa kwenye michezo ya riadha. Lakini kumekuwa na tatizo la viwanja vya muda mrefu, wachezaji hawa wanaenda kufanya mafunzo Arusha.
Ni lini sasa Serikali itatujengea kituo cha mafunzo kwa ajili ya kuendeleza vipaji hivyo? (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kusema katika majibu yangu ya swali la msingi ni kwamba tumezitaka Halmashauri zote nchini kutenga viwanja vya michezo ya aina mbalimbali hiyo ni hatua ya kwanza. Lakini hatua ya pili, Serikali tumeanzia na kujenga complex ya michezo kwa ajili ya michezo yote hapa Dodoma na nadhani tukiwa tunapita kuelekea Dar es Salaam tunaiona.
Mheshimiwa Spika, kimsingi niseme tu kwamba hata Sera yetu ya Michezo inaelekeza kwamba masuala ya viwanja vya michezo katika maeneo mbalimbali yanatakiwa ushiriki wa wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na makampuni na taasisi mbalimbali, hivyo niombe Halmashauri ishirikiane na wadau mbalimbali ili kuweza kuanzisha kituo cha michezo. Ahsante.