Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Primary Question

MHE. ABDALLAH H. ULEGA (K.n.y. MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA) aliuliza:- Mheshimiwa Spika, maeneo mengi ya Pwani huwa na madini mbalimbali. Je, eneo la Rufiji lina madini gani ili wananchi hawa washauriwe ipasavyo kutouza maeneo yao?

Supplementary Question 1

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Spika, asante sana, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jibu lake lenye kuleta matumaini ya kwamba siku moja na sisi watu wa Mkoa wa Pwani tunaweza tukapata madini ya dhahabu, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Swali la kwanza ninependa kujua ni lini sasa Wizara itaanza kukitumia kisima cha gesi kilichopo katika eneo la kijiji cha Kiparang’anda ndani ya Wilaya ya Mkuranga ili kiweze kupata na kutuletea faida watu wa Mkuranga na Taifa letu kwa ujumla?
Swali la pili, ningeomba Naibu Waziri wa Nishati na Madini anieleze Wilaya ya Mkuranga tunachimba madini ya aina ya mchanga, madini ambayo kwa sasa Mkoa wa Dar es Salaam hayachimbwi yanachimbwa tu Mkuranga. Je, Wizara iko tayari kushirikiana na sisi watu wa Mkuranga kuboresha ushuru na tozo mbalimbali ili madini haya yaweze kuleta tija kwa watu wa Mkuranga?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Ulega, tumeshirikiana na wewe sana katika suala la mchanga na wananchi wa Jimbo lako najua wananufaika sana, kwa hiyo, hongera kwa hilo Mheshimiwa Ulega.
Mheshimiwa Spika, labda nianze na lini kwamba gesi asilia itaanza kutumika maeneo ya Kiparang’anda. Shughuli zinazofanyika sasa katika eneo la Kiparang’anda ni ukamilishaji wa utafiti wa madini ya gesi asilia na Kampuni ya Moran and Promi inakamilisha sasa, Mheshimiwa Ulega madini haya ya gesi asilia yataanza kutumika kwenye eneo lako baada ya utafiti kukamilika mwezi Agosti, 2018 na wananchi wa Mkuranga wana matumaini makubwa, kwa hiyo jitihada zinafanyika ili kuhakikisha kwamba gesi asilia inakamilika na mwakani yataanza kutumika maeneo ya Kiparang’anda na maeneo mengine ya Dar es Salaam pamoja na Pwani kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na madini ya mchanga, Mheshimiwa Ulega nikupongeze sana, eneo la Pwani kwa ujumla wake jumla ya hekta kama 182 zinatumika sana kwenye uchimbaji wa madini ya mchanga pamoja na kokoto. Kinachotakiwa wakandarasi wote na nitumie nafasi hii kuwataka wakandarasi wote kwa niaba yako Mheshimiwa mwenye Jimbo la Mkuranga waanze sasa kulipa tozo za Serikali za Mitaa kwa mujibu wa sheria ambayo ni 0.3%. Lakini pia waanze sasa kushiriki katika shughuli za maendeleo kwa sababu ni takwa la kisheria, lakini nitumie nafasi hii kuwaagiza Wakurugenzi wote nchi nzima sasa waanze kuyataka makampuni yanayochimba mchanga, kokoto kuanza sasa kutoa ushuru katika Serikali za Mitaa ili wananchi wa Mkuranga na Tanzania nzima wanufaike kwa ujumla wake.