Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Lamadi ni mji ambao kijiografia unapanuka kwa kasi sana; na kwa kuwa Lamadi hiyo hiyo imeshakidhi vigezo ambavyo Mheshimiwa Waziri amevizungumza hapa, Wizara ya Ardhi imeshapima viwanja pale, miundombinu ya maji ipo, barabara zipo na Mheshimiwa Rais alipokuja alivutiwa sana na mji ule na akasema kwamba angependa uwe mji wa kibiashara, ufanye biashara kwa saa 24 kwa siku.
Je, Serikali haioni kwamba kama kuna kitu kinaitwa
hati ya dharura basi itumike kuufanya Mji wa Lamadi Mji mdogo ili kusudi iweze kuchochea maendeleo kwa wananchi badala ya kuendelea kuuacha hivi hivi ambapo baadaye unaweza ukaleta matatizo makubwa zaidi?
Swali la pili, kwa kuwa ukiangalia katika barabara inayotoka Mwanza kwenda Musoma, mji pekee ambao unakua zaidi ni Lamadi, Serikali haioni kwamba kuendela kuuachia kutangaza Halmashauri ya Mji Mdogo wa Lamadi itazidi kuleta matatizo makubwa zaidi kwa wananchi na kusababisha mpangilio ambao baadaye itakuwa ni tatizo kwa wananchi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Dkt. Chegeni mjukuu wa Mzee Mchengerwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, alivyosema kupeleka hati
ya dharura kwamba Mji wa Lamadi utangazwe kwa hati ya dharura, naomba nikuhakikishie Mheshimiwa Chegeni tulifika pale kwako Lamadi na mimi najua expansion ya mji ule unavyokua kwa kasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa zaidi ni kwamba kilio hiki tumekisikia na bahati nzuri Mheshimiwa Rais ameshaweka commitment pale alipokuwa site na bahati mbaya tulivyoangalia kuna baadhi ya changamoto ndogo ndogo ambazo zipo kuufanya mji ule tuutangaze rasmi. Naomba niseme kwamba jambo hili tunalichukua kwa pamoja, baadaye tujadiliane miongoni mwa zile changamoto zilizokuwepo tuziweke sawa ili mradi tuweze kufikia katika mpango ambao unastahiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo lingine kuhusu kuutangaza rasmi, Mheshimiwa Chegeni naomba tutakapokaa baadaye vizuri na bahati nzuri na Mheshimiwa Waziri wangu wa Nchi hapa yupo na amekusikia naye jambo hilo analiangalia kwa karibu zaidi tutafanya utaratibu wa kuona jinsi gani tufanye ili commitment ya Mheshimiwa Rais ameiweka pale basi mwisho wa siku waone kwamba kulikuwa na Dkt. Chegeni amepigania Mji wa Lamadi umeweza kupatikana na kuufanya mji wa kibiashara uweze kuendana na hadhi kwa kadri tutakavyoweza kuutangaza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kilio chako tumekisikia, tutaakaa pamoja, tutajadiliana pamoja nini tufanye sasa cha haraka kwa mustakabali wa Mji wa Lamadi ambao unakua kwa kasi. (Makofi)

Name

Desderius John Mipata

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkasi Kusini

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 2

MHE. DESDERIUS J. MIPATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Mji wa Namanyere ambao unakua pia kwa kasi na unapangwa vizuri, tumeshaomba uweze kupandishwa hadhi na kupata Mamlaka ya Mji wa Namanyere kwa maana ya Halmashauri ya Mji. Kamati ya Kitaifa ilishakuja ikaangalia na ikaona kwamba tuna vigezo vingi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua na wananchi wa Namanyere wajue, ni lini Serikali itapandisha hadhi Mji wa Namanyere ili tuweze kunufaika na miundombinu inayopaswa watu wa mjini, wanufaike?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mwaka 2016 nilikuwa na Wabunge, Mheshimiwa Mipata na Mheshimiwa Keissy pale tulipokuwa tunatembelea katika eneo lile na tumezunguka na ndiyo maana tukaamua kutuma timu. Waziri wangu akatuma ile timu ya haraka kupitia maeneo yote katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naomba niwaambie kwamba timu ile sasa wataalam ndiyo walikuwa wanahakiki kupitia vigezo mbalimbali baadaye mchakato utakavyoenda, utakapofika, basi utaambiwa kwamba Mji wetu wa Namanyere umefikia katika hatua gani.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwahakikishie kwamba lile jambo liko katika ofisi yetu linafanyiwa kazi baada ya ile timu yetu ya uhakiki kwenda kufanya kazi. Kwa hiyo, naomba tuvute subira tu kusubiri mchakato huo ukamilike halafu tutapata mrejesho kwa mustakabali wa Mji wa Namanyere.

Name

Pascal Yohana Haonga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 3

MHE. PASCAL Y. HAONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mji Mdogo wa Mlowo uliopo Wilaya Mbozi, tangu mwaka 2016 umetangazwa kuwa mji mdogo lakini hakuna shughuli yoyote pale inayoendelea kuonesha kwamba ni mji mdogo; bado vitongoji kama kawaida vipo na tayari ile asilimia 80 inayokusanywa na Halmashauri ya Wilaya inaendelea kukusanywa kama kawaida na asilimia 20 inarudi kwenye kijiji.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nijue ni lini rasmi sasa Mji Mdogo wa Mlowo utaanza kufanya shughuli zake kama Mji Mdogo na kama siyo kijiji kama ilivyokuwa kwa sasa japokuwa tangu mwaka 2016 tumeshapewa kuwa hadhi ya Mji Mdogo lakini shughuli zinazoendelea siyo za Mji Mdogo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, mji anaouzungumzia Mheshimiwa Haonga ni kweli ni mji ambao sasa hivi eneo lake bado lipo katika suala zima la vitongoji, lakini kuna utaratibu ule kwamba vile vijiji tufanye ule uchaguzi wa Serikali za Vitongoji, then wachague Mwenyekiti wa Vitongoji kwa mujibu wa taratibu, then atachaguliwa TEO, then mchakato huu utaenda.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anafahamu katika eneo lake kuna baadhi ya Vitongoji vingi sana havijafanya uchaguzi na hii nakumbuka alikuja ofisini kwangu tulikuwa tunatoa maelekezo kwa Mkurugenzi kwamba aangalie utaratibu wa kufanya yale maeneo ambayo uchaguzi haujafanyika, ziweze kufanya uchaguzi maeneo yote sawa sawa na eneo la Vwawa kule kwa Mbunge wetu wa Vwawa. Maana yake zikifanyika chaguzi zote, basi utaratibu mwingine utafanyika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo kubwa ni kwamba vile vitongoji vyote viwe na hadhi ya vitongoji na Wenyeviti wake wa vitongoji baadaye wachague Mwenyekiti wao Kitongoji, then achaguliwe TEO, baadaye ule mji sasa unakuwa na mamlaka kamili kufanya kazi yake. Kwa hiyo, ni jambo ambalo tutaendelea kutoa maelekezo kwa Mkurugenzi wetu, waendelee na michakato ile ya kufanya mamlaka ile inaweza kufanya kazi vizuri kama ilivyokusudiwa.

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 4

MHE. EZEKIEL M. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Isaka toka miaka ya 1990 imekuwa inajulikana kwamba ni bandari ya nchi kavu, uwekezaji mkubwa sana unafanyika pale na nchi jirani na hivyo ardhi imekuwa ni kitu adimu na uvamizi ni mkubwa. Kwa zaidi ya mwaka sasa wananchi wa Isaka walishaomba eneo hilo liwe mji mdogo na maombi yalishawasilishwa Wizarani lakini kumekuwa na ukimya. Nataka kujua ni hatua gani iliyofikiwa kwa lengo ya kuitangaza Isaka kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikia maswali mengi na karibu maswali yote yanaomba Miji Midogo. Tunazo Mamlaka za Halmashauri 185 kwa nchi nzima. Tunayo Miji Midogo mingi, mingine inafanya kazi na mingine imeshindikana hata kuanza; lakini pia ndiyo unasikia maswali haya mengi, Bwana Keissy, Mipata wanazungumzia Namanyere, ukimuuliza Mheshimiwa Kikwembe hapa, anazungumzia Majimoto, ukimuuliza Mheshimiwa Edwin Ngonyani anazungumzia kule kwake Namtumbo kule na Lusewa; wengine wanazungumzia Isaka. Kwa hiyo, hapa Waheshimiwa Wabunge wana maswali haya mengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jibu lake ni hili; ili uweze kuanzisha Mji Mdogo, lazima uangalie kwanza uwezekano wa kuweza kuwa na mapato ya ndani ya kujiendesha. Huanzishi tu halafu Serikali unataka ilete fedha ya kuendesha. Hizi Mamlaka 185 tulizonazo zinashindikana kupata fedha Serikalini kuziendesha; tunapoanzisha mamlaka nyingine tunaleta contradiction, kwa sababu kimsingi hizi mamlaka zinazaliwa na mamlaka mama. Halmashauri mama ndiyo inayozaa Mji Mdogo. Unaposema unaanzisha Mji Mdogo ukapeleka setup ya watumishi pale, maana yake Halmashauri mama ianze kugawana mapato na Halmashauri hii ndogo unayoianzisha ya Mji Mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa jambo hili mwanzo wake (genesis) yake ni huko huko kwamba je, hivi tunao uwezo wa kuweza kuanzisha mamlaka hii na ikajiendesha?Je, vyanzo hivi vikichukuliwa na Mji Mdogo, haviathiri Halmashauri mama? Ukimaliza stage hiyo sasa ukaona umejiridhisha, sasa omba.
Mheshimiwa Naibu Spika, cha msingi ninachoweza kushauri Waheshimiwa Wabunge, ili kuweza kwenda na hatua nzuri, hebu twende na stages kama inavyokwenda Lamadi. Kwamba Lamadi wameshafanya Mipango Mji wa ile sehemu; wameipima, lakini wameshajitosheleza katika huduma kama za maji, lakini wamekwenda mbali zaidi wanajenga mpaka barabara za lami; sasa ukifika mahali hapo; kwa mfano, nafahamu kwamba Lamadi sasa wawekezaji wanaojenga mpaka hoteli za kitalii maeneo yale; kwa hiyo, naamini haka kamji kanaweza kakajiendesha.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge niwasihi, hebu jambo hili twende nalo taratibu. Kama tuliahidi, hebu twende nalo taratibu kwa sababu uamuzi wake utazingatia sana tathmini ya tulikotoka, Miji Midogo tuliyoianzisha imefika wapi na hali ikoje? Ndiyo tufikie uamuzi wa kuamua ku-establish mamlaka hizi ndogo ndogo mpya.

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 5

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Halmashauri ya Nyang’wale imeanzishwa zaidi ya miaka minne na pakatokea kosa la kiuandishi katika GN yake, badala ya kuandikwa Nyang’hwale Makao yake Makuu Karumwa, ikaandikwa Makao Makuu Nyang’hwale na taarifa hii tumeshaileta na tayari leo zaidi ya miaka miwili GN ya Nyang’hwale mpaka sasa hivi hatujaipokea. Je, Mheshimiwa Waziri anatuambia nini sisi Wana-Nyang’hwale, kuna tatizo gani ambalo limekwamisha kuitoa GN hiyo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo makosa mengi, siyo kwako tu, lakini utaratibu na masahihisho yote yanafanywa na Katibu wa Bunge. Ikishatolewa ile GN, kama kuna marekebisho, inarudishwa na Katibu wa Bunge anaombwa kurekebisha. Bahati nzuri ya kwako iko tayari imerekebishwa na jana ilikuwa ofisini kwangu. Karibu uje uichukue. (Makofi)

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Mji mdogo wa Lamadi kwa muda mrefu umeidhinishwa kuwa Halmashauri ya Mji Mdogo:- Je, lini sasa utekelezaji wake utaanza?

Supplementary Question 6

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri juu ya process ya Miji Midogo na kwa kazi nzuri iliyofanywa na Serikali ya kufungua barabara ya lami kwenda Msumbiji inayopita katikati ya Jimbo la Mtama na ile inayokwenda Tunduru mpaka Songea, Miji ya Kiwalala, Mtama na Nyangao kasi yake ya kukua ni kubwa na hizo sifa ambazo Mheshimiwa Waziri alikuwa akizieleza zote tunazo.
Ni lini Serikali itakamilisha sasa mchakato wa kuitangaza miji hii midogo kuwa mamlaka kamili ambayo inajitegemea, badala ya kutaka tujumlishe yote kwa pamoja kama ambavyo Waziri anaeleza, nadhani twende case by case na kwa wale ambao wamekamilisha vigezo wapewe badala ya kusubiri wote kwa ujumla wake?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, ni kama tulivyosema pale awali, concern ya Mheshimiwa Nape ni kwamba ikiwezekana twende case by case, naomba nikuhakikishie kwamba tulivyoenda kufanya tathimini ya maeneo yote, maana yake hata tumefika sehemu nyingine kwa ajili ya watu wametu-invite makusudi kwenda kuangalia hiyo Miji Midogo. Tulipofanya hiyo ziara ndiyo maana tukatuma hiyo timu; na bahati nzuri hiyo timu imefanya kazi kubwa sana. Siyo muda mrefu sana, ile kazi ikikamilika sasa na baada ya kujiridhisha na haya mambo ambayo Mheshimiwa Waziri aliyazungumza kwamba suala zima la kuangalia vigezo vya kiuchumi eneo lile, basi tutatangaza maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuvute subira tu, kwa sababu kila jambo lina utaratibu wake na mchakato wake, kwa hiyo, tuvute subira tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo ambalo alizungumza, ni kweli linakua sana, basi tutaangalia jinsi gani tutafanya maeneo yatakayokuwa tayari, basi yatatangazwa kwa mujibu wa sheria.