Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Primary Question

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS aliuliza:- Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2009 Serikali ilikamata Meli ya Uvuvi MFV TAWARIQ, nahodha wake Tsu Chin Tai pamoja na watu wengine 36 walishtakiwa Mahakama Kuu kwa kesi ya Jinai Na. 38 ya mwaka 2009. Kwa amri ya Mahakama samaki tani 296.3 wenye thamani ya sh. 2,074,000,000/= waligawiwa bure. Aidha, meli hiyo ilizama ikiwa inashikiliwa kama kielelezo. Tarehe 23 Februari, 2012 watuhumiwa wawili walihukumiwa kifungo na walikata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo tarehe 25 Machi, 2014 waliachiwa huru na sasa ni miaka saba tangu meli hiyo ikamatwe. Je, Serikali itarudisha lini sh. 2,07,000,000/= ambazo ni thamani ya samaki na fedha ambazo ni thamani ya meli kwa Mawakili wa Nahodha wa Meli hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na mlolongo mrefu wa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mataifa mbalimbali duniani wanapozikamata meli kama hizi wanazitaifisha kwa ajili ya kujenga uchumi wa ndani ya nchi yao. Ajabu sisi meli ile tumeiacha imezama mahali (bandarini) ambapo hapana upepo, hapana wimbi wala hapana dhoruba yoyote na kupoteza thamani kubwa ya meli ile. Je, Serikali inatamka tamko gani kuhusu suala hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa washtakiwa wameingizwa hatiani: Je, utaratibu gani uliotumika kuwaachia huru mpaka muda huu wakawa wako nje? Ahsante.

Name

Andrew John Chenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA (K.n.y. WAZIRI WA SHERIA NA KATIBA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa ametolea mifano au ameelezea uzoefu wa nchi nyingine wanapokamata vyombo vya baharini au meli kama hizi. Kwanza, napenda tu kusema kwamba kwa Tanzania kufanya uamuzi ule waliouchukua imesaidia sana kukemea au ku-deter uvuvi haramu katika bahari zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia matukio ya aina hii kuanzia mwaka 2009 tangu uamuzi huu ulipochukuliwa, kwa kweli hata Wizara ya Uvuvi itakuwa ni shahidi na vyombo vyetu vinavyofanya doria katika bahari zetu, matukio ya aina hii yamepungua sana. Kwa hiyo, kwa kweli na sisi Tanzania kama nchi tumeweka mfano, tumeweka precedent ili nchi nyingine na watu wengine wenye masuala kama haya wasitumie bahari zetu kwa makosa na kuchezea rasilimali zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, kwamba ni utaratibu gani uliotumika katika kuwaachia huru watuhumiwa; kama nilivyoeleza, mwaka 2014 Mkurugenzi wa Mashtaka ali-enter nolle kupitia Kifungu cha 98 ambacho anayo mamlaka kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai na masuala mengine yaliyofuata hapo ilikuwa ni masuala ya diplomasia na waliweza kuachiwa huru.