Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 16 Justice and Constitutional Affairs Wizara ya Katiba na Sheria 136 2017-05-03

Name

Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Primary Question

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS aliuliza:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2009 Serikali ilikamata Meli ya Uvuvi MFV TAWARIQ, nahodha wake Tsu Chin Tai pamoja na watu wengine 36 walishtakiwa Mahakama Kuu kwa kesi ya Jinai Na. 38 ya mwaka 2009. Kwa amri ya Mahakama samaki tani 296.3 wenye thamani ya sh. 2,074,000,000/= waligawiwa bure. Aidha, meli hiyo ilizama ikiwa inashikiliwa kama kielelezo. Tarehe 23 Februari, 2012 watuhumiwa wawili walihukumiwa kifungo na walikata rufaa Mahakama ya Rufaa ambapo tarehe 25 Machi, 2014 waliachiwa huru na sasa ni miaka saba tangu meli hiyo ikamatwe.
Je, Serikali itarudisha lini sh. 2,07,000,000/= ambazo ni thamani ya samaki na fedha ambazo ni thamani ya meli kwa Mawakili wa Nahodha wa Meli hiyo?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Haji Khamis, Mbunge wa Nungwi kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 8 Machi,
2009 kikosi kazi kilichokuwa kikifanya doria katika ukanda wa kiuchumi wa Bahari Kuu ya nchi yetu (Exclusive Economic Zone) katika Bahari ya Hindi kilifanikiwa kukamata meli ya uvuvi iitwayo Na. 68 BU YOUNG ikivua katika bahari yetu bila kibali. Meli hiyo ilikuwa ikiongozwa na nahodha aitwaye TSU CHIN TAI, raia wa Jamhuri ya Watu wa China na alikuwa pamoja na wenzake 36. Pamoja na kuwa jina la meli hiyo ni No. 68 BU YOUNG, meli hiyo ilikuwa inatumia pia jina la TAWARQ 1 na TAWARIQ 2 ili kuficha jina halisi na kuendeleza kufanya uvuvi haramu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nahodha wa meli hiyo, yaani
TSU CHIN TAI na wenzake walishtakiwa Mahakama Kuu katika kesi ya jinai Na. 38/2009 ambapo nahodha Tsu Chin Tai na ZHAO HANQUING aliyekuwa wakala wa meli hiyo, walitiwa hatiani. Wawili hawa waliomba rufaa Mahakama ya Rufani ambapo mwaka 2014 Mahakama hiyo ilibatilisha na kufuta mwenendo mzima wa kesi baada ya kubaini kuwa kulikuwa na kasoro katika taratibu za kuwafungulia mashtaka. Kwa ufupi, hawakuwahi kushinda kesi na Mahakama ya Rufani haikuwahi kutamka kuwa wako huru kwa sababu hawana hatia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya uamuzi huo wa Mahakama ya Rufani, Mkurugenzi wa Mashtaka alifungua mashtaka upya katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na baadaye kuondoa mashtaka dhidi yao tarehe 22/8/2014. Baada ya miaka miwili, yaani 2016 Wakili Captain Bendera alifanya maombi namba 108/2016 katika Mahakama Kuu akimwakilisha Bwana Said Ali Mohamed Al Araimi ambaye hakuwa mmoja kati ya washtakiwa katika kesi ya msingi akiomba apewe meli au USD 2,300,000.00 kama thamani ya meli hiyo na sh. 2,074,249,000/= kama thamani ya samaki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama Kuu baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili, ilikubaliana na hoja za Jamhuri na kutupilia mbali maombi hayo. Katika uamuzi wake, Mahakama ilitamka yafuatayo, naomba kunukuu: “this application was uncalled for, superfluous and amounts to abuse of court process, thus devoid of any merit.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni suala la kisheria na wahusika wanaweza kuendelea kulishughulikia kupitia Mahakamani.