Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:- Mkoa wa Kigoma una madini ya chokaa, dhahabu, platinum na kadhalika:- Je, Serikali imechukua hatua gani kuendeleza utafutaji na uchimbaji wa madini katika mkoa huo?

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Swali la kwanza, katika Wilaya ya Kasulu katika kijiji cha Makere lakini pia katika Wilaya ya Kakonko wananchi wamekuwa wakipata kipato chao kwa kuchimba chokaa, lakini mara nyingi wamekuwa wakizuiliwa kufanya shughuli hiyo. Je, Wizara ya Madini na Wizara ya Maliasili iko tayari kukaa pamoja na wananchi hao ili kuweza kutatua tatizo hilo na kuwawezesha kuwa wachimbaji rasmi? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha inatenga eneo la wachimbaji wadogo ili kuepusha migogoro inayoweza kutokea baadaye?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa
Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Genzabuke wakati tunatenga eneo la Kakonko mwaka 2002 alitupa ushirikiano mkubwa sana. Kwa hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Genzabuke kwa kufuatilia maisha ya watu wa Kigoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na maswali yake mawili, la kwanza alitaka kujua namna sisi pamoja na taasisi ya maliasili tunavyoshirikiana ili kuwawezesha wananchi hawa kupata maeneo na kufanya uchimbaji kwa ajili ya kuongeza pato lao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge, Sheria ya Madini ya mwaka 2010 katika kifungu cha 95 pamoja na Sheria ya Mazingira zinakubaliana kwamba mtu yeyote anaweza akamilikishwa leseni katika eneo lolote ikiwa ni pamoja na maeneo ya reserve na hifadhi kinachotakiwa ni kupata kibali cha maandishi. Tumekuwa tukifanya hivyo Mheshimiwa Genzabuke ndiyo maana katika eneo la Makere kuna leseni 15 za uchimbaji wa chokaa, lakini katika maeneo mengine ya Lugufu kuna leseni saba za uchimbaji ambayo pia yako kwenye hifadhi. Kwa hiyo, hilo halina shida, lakini kama ulivyosema tutaendelea kukaa na wenzetu ili wananchi wa Kasulu na maeneo ya jirani waendelee kunufaika na uchimbaji wa madini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kutenga maeneo. Kama ambavyo nimejibu katika swali la msingi na ambavyo nimesema katika swali langu la nyongeza la kwanza ni kwamba tunaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo nchi nzima. Kwa sasa tumeshatenga maeneo saba katika Mkoa wa Geita na katika Mkoa wa Kigoma katika eneo linaloitwa Kinyo na Janda tutatenga maeneo hayo kwa ajili ya wachimbaji wadogo wa chokaa katika Wilaya ya Kasulu.

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:- Mkoa wa Kigoma una madini ya chokaa, dhahabu, platinum na kadhalika:- Je, Serikali imechukua hatua gani kuendeleza utafutaji na uchimbaji wa madini katika mkoa huo?

Supplementary Question 2

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kuna baadhi ya maeneo nchini mfano Wilaya za Manyoni na Bahi imebainika kuwa kuna madini ya uranium na inasemekana kwamba madini haya yana thamani kubwa sana na yanahitajika maeneo mbalimbali nchini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuchimba madini hayo ili wananchi wa maeneo yale pamoja na Serikali ifaidike? Ahsante.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nilieleza Wakala wa Jiolojia wanafanya utafiti wa kubaini mbale, jiokemia, jiofizikia na jiolojia ili kujiridhisha kama maeneo fulani yana madini ya aina gani. Ni kweli kabisa katika maeneo ya Manyoni, Bahi pamoja na maeneo mengine ya Singida ikiwemo eneo la Sekenke, GST wamekuwa wakifanya utafiti. Sasa hivi wanakamilisha shughuli za utafiti kubaini kama hiyo uranium ambayo inaonekana inaweza ikatathminiwa ikachimbwa kwa kiwango gani.
Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika maeneo ya Bahi na maeneo mengine ya Manyoni pamoja na Sekenke yapo madini ya dhahabu na madini megine. Bado GST wanajiridhisha lakini mara baada ya kukamilisha maeneo haya yatatengwa kwa ajili ya wachimbaji wadogo ili waweze kuchimba sasa kwa uhakika. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira, zoezi la ukamilishaji wa utafiti la GST likamilike na linatarajiwa kukamilika mwezi Desemba mwaka huu.