Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 14 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 113 2017-04-28

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Mkoa wa Kigoma una madini ya chokaa, dhahabu,
platinum na kadhalika:-
Je, Serikali imechukua hatua gani kuendeleza utafutaji na uchimbaji wa madini katika mkoa huo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Mkoa wa Kigoma una madini ya aina mbalimbali yakiwemo madini ya chokaa, chuma, cobalt, dhahabu, galena, nickel, shaba na platinum.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) ilifanya utafiti wa awali wa madini nchi nzima na kuandaa ramani za jiolojia nchini. Utafiti huo utasaidia kutangaza fursa za uwepo wa madini yanayogunduliwa ili wawekezaji wa ndani na nje ya nchi waweze kuwekeza katika tafiti za kina na uchimbaji wa madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1959 hadi 2010 Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) walifanya utafiti wa jiolojia katika Mkoa wa Kigoma na kutengeneza ramani za jiolojia 22 kwa nchi nzima na hasa katika Mkoa wa Kigoma. Kati ya mwaka 2013 hadi 2014, GST kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ikiwemo kampuni ya Beak Consultants GmbH ya Ujerumani na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam walifanya utafiti wa awali kubainisha uwepo wa madini mbalimbali Mkoani Kigoma kama ifuatavyo:-
Madini ya tin katika maeneo ya Bwuhinika, Kabogo, Kapalagulu na Lugufu; madini ya shaba katika maeneo ya Gagwe, Kampisa na Nyamori; madini ya barite katika eneo la Ilagala; chumvi katika eneo la Uvinza; dhahabu katika maeneo ya Isabika, Lumbwa, Lusahunga pamoja na Mwiruzi; madini ya agate katika maeno ya Kabingo, Kasulu, Keza na Nkuba; madini ya nickel katika eneo la Kapalagulu na madini ya chokaa katika maeneo ya Lugufu, Makere, Matiaso pamoja na Kasuku. Utafiti wa kina unahitajika ili kubaini kiasi halisi cha mashapo yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwezi Machi 2017, Mkoa wa Kigoma ulikuwa na jumla ya leseni 15 za utafutaji wa madini ya dhahabu, leseni 20 za utafutaji wa madini ya shaba na leseni 2 za utafutaji madini ya platinum. Vilevile kuna leseni 25 za uchimbaji mdogo wa madini ya dhahabu na leseni 118 za uchimbaji mdogo wa madini ya chokaa, kadhalika kuna leseni 716 za uchimbaji mdogo wa madini ya shaba katika maeneo mbalimbali Mkoani Kigoma.