Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Boniphace Nyangindu Butondo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kishapu

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:- Je, lini ujenzi wa wodi za wagonjwa, nyumba za Madaktari, maabara na mortuary katika Vituo vya Afya vya Mwanhalanga na Negezi utakamilika?

Supplementary Question 1

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kuipongeza Serikali kwa majibu mazuri kuhusiana na miradi hii miwili Mwanhalanga na Ukenyenge.

Mheshimiwa Spika, ninaomba tu kushukuru kwamba shilingi milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Ukenyenge zilijenga yale majengo matano lakini upungufu bado ni mkubwa sana na hivyo kupelekea Kituo hiki kuendelea kubaki na kutokuwa na hadhi kama Kituo cha Afya. Tunahitaji majengo kwa ajili ya wodi za akina mama na akina baba lakini tunahitaji pia walkways kwa baadhi ya Wodi ambazo zitakuwa zinaunganishwa na hizi njia za kuwafikisha Madaktari na wagonjwa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mwanhalanga. Kituo hiki cha afya kina majengo mawili tu na bado wagonjwa ni wengi sana. Ni lini Serikali itakwenda kujenga majengo maalum kwa ajili ya wodi za akina mama, wodi za akina baba, mortuary pamoja na nyumba za watumishi ili tuongeze ari ya watumishi kutenda kazi katika maeneo haya? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Butondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza napokea pongezi zake kwa Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo kwa kweli imefanyika katika Sekta ya Afya kwa ujenzi wa Vituo vya Afya kikiwemo hiki Kituo cha Afya cha Negezi ambacho kimepokea shilingi milioni 500. Ninamhakishia tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunatambua majengo haya bado hayatoshi, hayajakidhi mahitaji, bado tunahitaji wodi, bado tunahitaji mortuary na majengo mengine.

Mheshimiwa Spika, safari ni hatua Mheshimiwa Mbunge, Serikali inaendelea kutenga fedha kwenye bajeti, tuhakikishe kwamba fedha hizi zinapelekwa kwa ajili ya kukamilisha miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Spika, pia kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mwanhalanga, tunafahamu, tulishapeleka fedha lakini bado kuna majengo ambayo tumeshaweka mpango mkakati kwa ajili ya kutenga fedha ya ukamilishaji. Ahsante.

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:- Je, lini ujenzi wa wodi za wagonjwa, nyumba za Madaktari, maabara na mortuary katika Vituo vya Afya vya Mwanhalanga na Negezi utakamilika?

Supplementary Question 2

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Mgeta kimejengwa toka mwaka 2018 mpaka leo kimejengwa mortuary imekamilika hakina majokofu manne ya mortuary. Ni lini Serikali itapeleka majokofu manne ya mortuary pamoja na kwamba vituo hivyo vilipewa shilingi milioni 400 ya kujenga na milioni 300 ya vifaa vya tiba...

SPIKA: Umeshauliza swali Mheshimiwa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Mgeta kimejengwa, kimekamilika, kimeanza kutoa huduma lakini jengo la kuhifadhia maiti limekamilika, tayari Serikali imeshapeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Halmashauri ya Bunda. Moja ya kazi ambayo itafanyika ni kununua jokofu kwa ajili ya kuhifadhia maiti katika kituo hiki cha Mgeta. Ahsante.

Name

Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:- Je, lini ujenzi wa wodi za wagonjwa, nyumba za Madaktari, maabara na mortuary katika Vituo vya Afya vya Mwanhalanga na Negezi utakamilika?

Supplementary Question 3

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Magendo, Kibaha Vijijini tumepokea jokofu la kuhifadhia maiti lakini mortuary haijajengwa; je, lini tutapata pesa kwa ajili ujenzi?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo kuwa Serikali ilishatoa maelekezo kwa Halmashauri zetu kote nchini, kwamba Mheshimiwa Rais anapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya, lakini anapopeleka fedha kwa ajili ya vifaatiba, kuna baadhi ya miundombinu ambayo iko ndani ya uwezo wa mapato ya ndani ya Halmashauri kama majengo ya mortuary.

Mheshimiwa Spika, natumia fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumuelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kibaha, kutenga fedha kwenye mapato ya ndani kujenga jengo la mortuary ambalo ni jengo la gharama ya kawaida kabisa ili wananchi waendelee kupata huduma katika eneo hilo. Ahsante.(Makofi)

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:- Je, lini ujenzi wa wodi za wagonjwa, nyumba za Madaktari, maabara na mortuary katika Vituo vya Afya vya Mwanhalanga na Negezi utakamilika?

Supplementary Question 4

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Susuni na Mwema zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, hazina kabisa Kituo cha Afya na hivyo kusababisha wananchi kutembea kuja kutafuta huduma Tarime Mjini. Nataka kujua ni lini Serikali itapandisha hadhi Zahanati ya Kiongera ambayo imekarabatiwa ili kuwa Kituo cha Afya na kuweza kurahisisha huduma kwa wananchi hawa?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante, ujenzi wa vituo vya afya katika Kata, tunajenga kimkakati, kwanza kwa kufanya tathmini ya vigezo kwa maana ya idadi ya watu, umbali kutoka kituo kingine, pia maeneo yale ambayo ni magumu kufikika. Kwa kuwa, Kata hii ya Susuni na Mwema hatujapata tathmini yake ya kutosha, naomba tuichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge tukafanye tathmini tuone kama inakidhi vigezo, tuziingize kwenye mpango mkakati, aidha kupandisha hadhi zahanati au kufanya ujenzi katika Kata hizo, ahsante.