Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Saashisha Elinikyo Mafuwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kuelekeza taasisi zake kununua mashine na vipuri katika kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools?

Supplementary Question 1

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, na ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa sasa Serikali imeridhia kwamba taasisi zake zikanunue vyuma pamoja na vipuri kwenye kiwanda hicho;

Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kuweka mpango mzuri wa kutumia chuma cha Liganga ambacho Serikali inaendelea na mchakato wa kuzalisha ili chuma hicho kitumike kuzalisha vyuma kwa ajili ya taasisi zetu za Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Halmashauri ya Wilaya ya Hai imepeleka maombi ya kupewa eneo kwa ajili ya kuanzisha Mji Mdogo wa Kibiashara Njia Panda ya kwenda Machame. Ninaomba kufahamu, Serikali imefikia wapi katika mpango huo wa kutupa eneo la kibiashara Njiapanda ya Machame?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, ni kweli moja ya mikakati ya Serikali ni kuona rasilimali zetu nchini zinatumika kuzalisha bidhaa ambazo tunahitaji kuzitumia na hasa kwenye hizi bidhaa za chuma ambazo tunatumia fedha nyingi sana kuagiza chuma kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Serikali tunavyoendelea kutimiza na kukamilisha uanzishwaji na utekelezaji wa Mradi wa Liganga na Mchuchuma tunaamini hii ndio itakuwa malighafi itakayotumika na kiwanda hiki cha KMTC.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari kuna hatua zimeshafanyika ikiwa ni pamoja na kulipa fidia kule Mchuchuma na Liganga, na sasa tunakamilisha majadiliano na wawekezaji ili tuanze kuchimba chuma na kuhakikisha inatumika katika viwanda vyetu kikiwemo KMTC.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusu swali la pili; ni kweli Mheshimiwa Mbunge amekuwa akifuatilia sana kuhakikisha eneo hili la KMTC ambalo ni eneo kubwa wenzetu wa Halmashauri ya Hai wanapata eneo la kujenga Mji Mdogo katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari Serikali tumeshaanza kujadiliana na kupitia NDC ambao wameshaweka master plan ili kuona namna ya kua-accommodate maombi hayo ya Mheshimiwa Mbunge na wana Hai. Katika mpango huo tutaona nini tutawapa na wafanye shughuli gani zinazoendana na mahitaji mahsusi ya Kiwanda hiki cha KMTC, nakushukuru sana.