Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Simai Hassan Sadiki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nungwi

Primary Question

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI aliuliza:¬- Je, sababu zipi zimekwamisha ujenzi wa ukuta maeneo yanayoathiriwa na Bahari Nungwi?

Supplementary Question 1

MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu ya Serikali, ikumbukwe ya kwamba mwaka 2020/2021 niliuliza suala hili hili. Mwaka 2021/2022 nikauliza tena suala hili hili na nikajibiwa kwamba katika bajeti ile litatengwa Fungu Maalum kwa ajili ya kwenda kujenga ukuta ule. Mwaka 2022/2023 nimeishauliza tena suala hili ndiyo kwanza milioni mia sita zimetengwa kwa ajili ya utafiti. Ninachotaka kujua ni lini Utafiti huu utaanza wakati ambapo milioni sita hiyo inauwezo wa kutosheleza kujengea huo ukuta? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili. Kwa kuwa Wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, harakati zao za kiuchumi zimeegemea zaidi katika shughuli za uvuvi na utalii. Mambo ambayo yamekuwa yakitaja ni miongoni ambayo yanapelekea kuharibu na kupelekea athari za mabadiliko ya tabiachi. Je, Serikali ina mpango gani ya kuokoa mazingira ya bahari yaliyosababishwa kutokana na athari za uvuvi na utalii? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Simai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, changamoto yetu kubwa katika ujenzi wa ukuta huu ulikuwa ni kuweza kuanza kupata fedha za kuanza kufanya tathimini ya awali. Kwa kuwa sasa fedha zimeishapatikana, tulichokifanya tayari tumeishawasiliana na tumeishawasilisha andiko letu kwa wenzetu Wakala wa Majengo. Kwanza kwa ajili ya kutufanyia Michoro ama Ramani kwa ajili ya aina ya ukuta ambao unatakiwa.

Mheshimiwa Spika, kuna kuta za aina nyingi, kuna gabrion wall, kuna zile slope, kuna zile vertical, kuna blocks. Sasa tunataka tufanye utafiti tujue ni aina gani ya ukuta ambao wananchi wa pale utaweza kuwasaidia lakini pia umesema tuwatengenezee ukuta ambao utaweza kuwasaidia kuzuia maji lakini pia waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi kama ambavyo Wananchi wako hivyo. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa kwa kuwa taratibu tumeishazianza sasa hivi tunakwenda kuanza hii tathimini ili lengo na madhumuni tuwapelekee ukuta utakao wasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli shughuli zetu za uvuvi lakini na shughuli za utalii zimekuwa zikiathiri mazingira hasa maeneo ya bahari na maeneo ya fukwe. Tayari tumeona kwamba shughuli za uvuvi haramu, shughuli za uvuvi usiyokuwa rasmi lakini shughuli za ulimaji wa mwani na shughuli nyingine zinazofanyika pembezoni ama ndani ya bahari zinaathiri mazingira. Lakini la kwanza tumeanza kutoa elimu kwa Wananchi ili lengo na madhumuni Wananchi wafahamu ni aina gani ya uvuvi ni aina gani ya shughuli ambazo wanatakiwa wafanye kwenye bahari?

Mheshimiwa Spika, lakini tumeanza kufanya doria, tunashirikiana na wenzetu wa Thumka, wenzetu wa Mji Mkongwe, wenzetu wa Mlemba Conservation na wenzetu wengine kupitia Wizara ile ya Uchumi wa Bluu. Lakini kikubwa zaidi tumeanza kuchukua hatua zikiwemo za kuangamiza nyavu na vifaa vyote vinavyoweza kuweza kuathiri mazingira ya bahari, nakushukuru. (Makofi)