Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 9 Finance Wizara ya Fedha 129 2023-09-08

Name

Eng. Ezra John Chiwelesa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. NDAISABA G. RUHORO K.n.y. MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza:-

Je, nini mpango wa Serikali katika kunusuru uchumi wa nchi kutokana na ukosefu wa fedha za kigeni, hususani Dola ya Kimarekani?

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA FEDHA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za muda mfupi, wa kati na za muda mrefu katika kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa fedha za kigeni, hususani dola ya Kimarekani hapa nchini. Changamoto hiyo imesababishwa na athari za mgogoro wa vita kati ya Ukraine na Urusi; kuimarika kwa shughuli za kiuchumi na kijamii baada ya UVIKO-19; na mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Spika, sababu nyingine ni utekelezaji wa sera za fedha ambayo inalenga kupunguza ukwasi katika uchumi wa nchi mbalimbali ikiwemo Marekani katika kukabiliana na masuala ya mfumuko wa bei. Kwa ujumla matukio hayo yameathiri mnyororo wa uzalishaji, usambazaji na uhitaji wa bidhaa na huduma katika soko la dunia.

Mheshimiwa Spika, hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali katika kupunguza athari na changamoto za upatikanaji wa fedha za kigeni ni pamoja na:-

(a) Kuongeza kiwango cha kuuza fedha za kigeni katika soko la fedha za kigeni, ambapo kati ya Machi, 2022 na Agosti, 2023 Benki Kuu ya Tanzania imeuza katika soko la fedha za kigeni zaidi ya dola za Kimarekani milioni 500;

(b) Kuongeza vyanzo vya upatikanaji wa fedha za kigeni ikiwemo ununuzi wa dhahabu;

(c) Kutekeleza mikakati ya kuongeza mauzo ya nchi za nje na kuzalisha bidhaa mbadala wa zile zinazoagizwa kutoka nje ya nchi; na

(d) Kuendelea kushirikisha benki za biashara, maduka ya kubadilisha fedha za kigeni, pamoja na wadau wengine katika kuimarisha sheria, kanuni na miongozo mbalimbali ya usimamizi wa fedha za kigeni hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto zilizojitokeza, hali ya upatikanaji wa fedha za kigeni nchini imeendelea kuwa himilivu ambapo akiba ya fedha za kigeni ilifikia dola za Marekani milioni 5,246.7 mwezi Julai 2023, kiasi kinachotosheleza uagizaji wa bidhaa na huduma kutoka nje ya nchi kwa takriban miezi 4.7 ikilinganishwa na malengo ya miezi minne.