Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 3 Community Development, Gender and Children Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum 43 2023-08-31

Name

Maryam Azan Mwinyi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Chake Chake

Primary Question

MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kufuatilia mila potofu za kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama hasa Manyara na Arusha?

Name

Dr. Dorothy Onesphoro Gwajima

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi kuhusu mpango gani Serikali tunao kufuatilia mila potofu za kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama hasa mikoa ya Manyara na Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua kuwa kuna mila zenye faida ambazo zinapaswa kuendelezwa na mila zenye kuleta madhara ambazo Mheshimiwa Mbunge ameziita “Mila potofu” ikiwemo mila ya kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama. Mila hii ina madhara kwa kuwa inachochea ukatili wa kihisia, ndoa za utotoni na ina mnyima mhusika haki yake ya msingi ya kumchagua mwenza wa kuishi naye umri utakapofika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutokomeza mila za aina hiyo, Serikali imeandaa utaratibu wa kufanya majadiliano kuhusu masuala ya kimila na majadiliano haya yanahitaji umakini mkubwa katika kuyajadili. Hivyo basi, Wizara imeandaa mwongozo wa Taifa wa uendeshaji majadiliano kuhusiana na mila na desturi zenye madhara kwa jamii wa mwaka 2022. Majadiliano hayo yanakuwa ni jumuishi yanayohusisha viongozi wa mila, viongozi wa dini, wazee maarufu na wataalam waliopo katika ngazi ya jamii ili kuja na ujumbe mahsusi wenye lengo la kutokomeza mila zenye madhara ikiwa ni pamoja na kuwekeza mke akiwa tumboni mwa mama yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa wito kwa Wataalam wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii waliopo ngazi za Jamii kuandaa majukwaa ya kuongoza majadiliano haya kuhusu mila hiyo yenye madhara na kuja na ujumbe mahsusi utakaotumika kutoa elimu ikiwa ni kwenye nyumba za ibada pia na kwenye redio mbalimbali. Ahsante.